Sunday, July 19, 2015

Damu Ya Ukoo Wangu: Sehemu ya 1


Utangulizi...
    Katika hospitali kuu ya Muhimbili karibu na wodi ya wagonjwa mahututi, nilisimama huku nikishindwa kuelewa kama kweli yalikuwa yakitokea au ndiyo mipango ya Mungu ilikuwa ikitimia. Niligeuka kujaribu kuona kama wenzangu niliokuwa nimeongozana nao bado walikuwa na matumaini au kama walishayapoteza kama mimi.
    Dada wa mke wangu ambaye alikuwa akiitwa mama Saida lakini kutokana na unene wake wengi tulikuwa tukimuita mama Bonge pamoja na mdogo wake mke wangu aliyekuwa akiitwa Jenifer tukilifupisha jina lake na kumuita Jeni, hawakuweza kuyazuia machozi kuwatoka. Walikuwa wamejiinamia kwenye benchi huku vitenge vyao vikiwa mikononi mwao kwa ajili ya kujifuta machozi. Mdogo wangu wa kike, jina lake Tumsifu alikuwa kati kati yao akijitahidi kuwapa moyo kuhusu mdogo wao.
    Mdogo wangu Shukuru yeye alikuwa karibu yangu akitembea hapa na pale kujiongezea ujasiri. Hao ndio niliokuwa nimeongozana nao na hakukuwa na mtu aliyeonesha kuwa na matumaini kuhusu kupona kwa mgonjwa wetu ambaye alikuwa mahututi. Wote walikuwa wakisubiri kudra za mwenyezi Mungu kumponyesha mgonjwa wetu.
    Pilika pilika za watu katika hospitali hiyo ya taifa hazikuisha. Wauguzi, madaktari, wagonjwa na ndugu wa wagonjwa mbalimbali walikuwa wakipishana kuelekea huku na kule mbele ya eneo tulilokuwepo. Sura za huzuni ndizo zilizokuwa zikionekana eneo hilo isipokuwa kwa madaktari na wauguzi waliozoea kuona hali mbaya za binadamu.
    Baada ya muda mrefu kupita mimi na Shukuru tukiwa tumesimama wakati mama bonge, Jeni na Tumsifu wakiwa wamejiinamia kwenye benchi karibu na wodi ya wagonjwa mahututi, wakapita watu wakivuta machela moja na juu ya machela hiyo alikuwepo kijana mmoja akiwa anavuja damu kichwani naye uso wake ulikuwa huonekani kutokana na lijeraha likubwa alilolipata. Wauguzi wawili walikuwa wakijaribu kuizuia damu hiyo huku akiendelea kupelekwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi. Wagonjwa waliokuwa wakipelekwa kwenye wodi hiyo kweli walikuwa na hali mbaya na mgonjwa wetu naye, hakuwa wa kutofautishwa.
    Baada ya kumuona kijana yule, niliangalia chini nikiwaza kama ingekuwa vema kwangu kufanya ningechopaswa kufanya au kuwa na huzuni, kusubiria neema ya Mola bila ya kujishughulisha kama wengine. Nilijua fika kwamba mke wangu alikuwa katika hali mbaya na juhudi za madaktari zisingeweza kuzaa matunda yoyote. Walikuwa wakijitahidi kumshughulikia kwa elimu yao ya kisayansi lakini mimi nilijua sayansi iliyohitajika ilikuwa ile ya giza, sayansi ya kiroho na si ya kimwili.
    Nilitamani kuingia wodini nione jinsi matibabu yalivyokuwa yakiendelea lakini nilishindwa kutokana na mlango kufungwa. Akili ya ghafla iliniingia nami nikaifuatilia kwa haraka ile machela mpaka walipofika mlangoni ambapo ndugu wa yule kijana, mimi nikidhaniwa mmoja wao tukaombwa na muuguzi tuondoke eneo lile kwani tayari alishawafikia madaktari. Wale ndugu walianza kuondoka naye muuguzi akajua wote tungeondoka lakini mimi niliendelea kusubiri hata walipofungua mlango kumuingiza yule kijana nikalazimisha kuchungulia na kuona mke wangu akiwa amezungukwa na madaktari na wauguzi huku wagonjwa wengine wakiwa wameachwa kando. Niliamini hiyo ilitokana na hali yake kuwa mbaya zaidi kuliko wengine lakini haikupita hata nusu dakika kabla sijaombwa kuondoka eneo lile tena kwa sauti ya kukaripiwa.
    Nikiwa nasogea mbali na eneo hilo, hasira zilianza kunipanda kichwani na kuanza kujiwazia.
    ‘Umeniulia kopiraiti yangu nikakuvumilia na sasa unataka unichukulie na mke wangu?’
   Nilitamani niweze kumfuata Shukuru ili tuweze kushauriana juu ya nini cha kufanya lakini ubinafsi ulikuwa umenitawala. Nililichukulia jambo hilo kama mashindano na nilitaka kuwa timu ya peke yangu. Niliutaka ushindi zaidi ya kitu chochote nao haukuwa ushindi wa peke yangu bali hata adui yangu naye angeshinda kwa namna hiyo. Ama si hivyo basi tungeshindwa wote, yalikuwa ni mashindano ya kipekee na niliokuwa nikishindana nao hawakuwa watu wa kawaida.
    Bado nikiwa sijapata maamuzi ya moja kwa moja nikamuona daktari mmoja akitoka kwenye wodi ile ya wagonjwa mahututi akiwa ameinamisha kichwa chini. Nilipoziona ndevu na sharubu zake pamoja na mawani yake machoni niliweza kumgundua kuwa ndiye daktari aliyekuwa akimuhudumia mke wangu. Sasa alikuwa ametoka nje nami nikapata wazo la ghafla kuwa alikuwa amemaliza kazi yake lakini kabla sijamfuata kumuulizia hali ya mke wangu nikamuona muuguzi mmoja akimfuata na kusimama mbele yake. Alionesha kumbembeleza kitu fulani na daktari huyo alitingisha tu kichwa huku akitanua mikono yake kufanya ishara ya kutokujua cha kufanya. Niliogopa sana na nikajikuta nikielekea pale walipo kwa haraka lakini hatua mbili kabla ya kuwafikia, nilijihisi nikipooza(kuparalaizi) miguu nilipoona machela ikitoka wodi ile nayo ikiwa na mtu aliyefunikwa shuka jeupe mwili mzima.

 [Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi