Baada ya shangwe hizo
na wosia, Kayumbas anaingia ndani na kubadili nguo zake akivaa nguo chakavu
kidogo maalumu kwa kushindia. Kisha anamsaidia mama yake kutayarisha mboga za
majani kwa ajili ya kuziuza kwa kuzitembeza. Anapomaliza kumpangia mboga hizo
yakiwemo majani ya maboga, kisamvu, matembele na spinachi kwenye beseni
analotumia mama yake kubebea, Kayumbas anarudi ndani na kubadili tena nguo kwa
ajili ya kwenda kumchukua mdogo wake aliyeko shule ya awali umbali wa maili
kadhaa.
Kayumbas anapotoka
tayari kwa kumfuata mdogo wake huyo aliyeitwa Majaliwa, mama yake ambaye alikuwa
akibandika maji baada ya kumaliza kumfunga kamba kuku aliyemnunua kwa mmoja wa
majirani anamwambia,
"Yani mana oko
nafurahishwa sana na juhudi zako. Naamini Iruwa hatakutupa
kamwe."
"Mama, nitajituma
kwa juhudi zote na mengine nitamuachia Mungu."
"Ila Kayu..."
Anamuita na kumvuta
hadi anapokuwa karibu naye, anamshika mikono yote miwili na huku akimuangalia
machoni anamuambia kwa upole.
"Unajua ya Iruwa
mengi, ila naomba moyo huu wa kuwasaidia wadogo zako uendelee nao usije
ukachoka hata kama Iruwa atatuchukua mapema mkabaki ninyi wenyewe."
"Mamaaa..."
Anaita Kayumbas kwa sauti ya kulalamika na anapomuona mama yake akimsikiliza,
anaendelea, "uthitheme hivyo mama."
"Usiogope Kayu mana
oko, nakuambia tu ujue ninachokutakia katika maisha."
"Thawa mama lakini
hata hivyo thiyo vizuri. Naweza kwenda mama?"
"Safari njema mana
oko."
Shughuli zinaendelea na
inapofika saa mbili kasorobo usiku, baba Kayumbas anarudi nyumbani na kukuta
familia yake ikiwa imekusanyika sebuleni na nyuso za furaha zikiwa
zimewatawala. Baada ya kupokea salamu mbali mbali kutoka kwa familia yake,
anamchukua Mjanja aliye mdogo kuliko wote na kumrusha juu mara mbili kisha
anambusu na kumuweka chini.
Mama Kayumbas
anatazamana na Kayumbas na kisha kumtazama baba Kayumbas hadi anapofanikiwa
kuangaliana naye na kusema,
"Baba Kayumbas
umesikia alichokifanya mwanao?"
"Mm.. mmwa...mwanangu
yupi huyo?" Anauliza baba Kayumbas akiwa na shauku ya kutaka kujua ambapo
mama Kayumbas anamgeukia Kayumbas na kumwambia,
"Kayumbas hebu
mwambie baba yako habari nzuri naye afahamu."
"Enhee, uuu.. umee..
umeokota aaa..aalmasi nini?" Anaingilia kati baba Kayumbas akitaka
kumuharakisha Kayumbas kumfahamisha lakini anaonywa na mama Kayumbas.
"Eeeh eeh baba Kayumbas!
Utawafundisha watoto kuwaza hela za bahati nasibu. Lazima utoke jasho ndiyo
ufanikiwe. Siyo kwa kuokota."
"Natania tu. Ka si..
si.. si uuu..uumemuuuelewa mama yako?" Baba Kayumbas anajaribu kuufuta
usemi wake na kutaka kujua kama Kayumbas aliyekuwa akimuita 'Ka' kwa ajili ya
kumrahisishia maongezi, alikuwa ameielewa falsafa ya mama yake ambapo Kayumbas
akamjibu,
"Ndiyo baba
nimemuelewa."
"Enhee, ni..ni..ambie
hizo ha... ha..habari."
"Nimefaulu mtihani
wa taifa wa daratha la nne."
"Enheee, heee ni..ni..nilikwambia
mimi mmm..mm..ma Ka. Anasimama kidogo na kwa sauti iliyojaa msisitizo anasema, "Mtoto
tumepata." Kimya kingine cha sekunde kadhaa na kisha anamalizia, "Ho..ho..hongera
sana mmm..m..mwanangu, yani ho..ho..hongera sana."
"Athante baba."Anaitikia
Kayumbas na kisha baba yake anauliza,
"Eee enhee, kwa
hiyo uuu..uu..umekuwa wa ngapi shuleni?"
[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]
No comments:
Post a Comment