Wednesday, August 12, 2015

Roho ya Kayumbas: Sehemu ya 3



Baada ya shangwe hizo na wosia, Kayumbas anaingia ndani na kubadili nguo zake akivaa nguo chakavu kidogo maalumu kwa kushindia. Kisha anamsaidia mama yake kutayarisha mboga za majani kwa ajili ya kuziuza kwa kuzitembeza. Anapomaliza kumpangia mboga hizo yakiwemo majani ya maboga, kisamvu, matembele na spinachi kwenye beseni analotumia mama yake kubebea, Kayumbas anarudi ndani na kubadili tena nguo kwa ajili ya kwenda kumchukua mdogo wake aliyeko shule ya awali umbali wa maili kadhaa.
Kayumbas anapotoka tayari kwa kumfuata mdogo wake huyo aliyeitwa Majaliwa, mama yake ambaye alikuwa akibandika maji baada ya kumaliza kumfunga kamba kuku aliyemnunua kwa mmoja wa majirani anamwambia,
"Yani mana oko nafurahishwa sana na juhudi zako. Naamini Iruwa hatakutupa kamwe."
"Mama, nitajituma kwa juhudi zote na mengine nitamuachia Mungu."
"Ila Kayu..."
Anamuita na kumvuta hadi anapokuwa karibu naye, anamshika mikono yote miwili na huku akimuangalia machoni anamuambia kwa upole.
"Unajua ya Iruwa mengi, ila naomba moyo huu wa kuwasaidia wadogo zako uendelee nao usije ukachoka hata kama Iruwa atatuchukua mapema mkabaki ninyi wenyewe."
"Mamaaa..." Anaita Kayumbas kwa sauti ya kulalamika na anapomuona mama yake akimsikiliza, anaendelea, "uthitheme hivyo mama."
"Usiogope Kayu mana oko, nakuambia tu ujue ninachokutakia katika maisha."
"Thawa mama lakini hata hivyo thiyo vizuri. Naweza kwenda mama?"
"Safari njema mana oko."
Shughuli zinaendelea na inapofika saa mbili kasorobo usiku, baba Kayumbas anarudi nyumbani na kukuta familia yake ikiwa imekusanyika sebuleni na nyuso za furaha zikiwa zimewatawala. Baada ya kupokea salamu mbali mbali kutoka kwa familia yake, anamchukua Mjanja aliye mdogo kuliko wote na kumrusha juu mara mbili kisha anambusu na kumuweka chini.
Mama Kayumbas anatazamana na Kayumbas na kisha kumtazama baba Kayumbas hadi anapofanikiwa kuangaliana naye na kusema,
"Baba Kayumbas umesikia alichokifanya mwanao?"
"Mm.. mmwa...mwanangu yupi huyo?" Anauliza baba Kayumbas akiwa na shauku ya kutaka kujua ambapo mama Kayumbas anamgeukia Kayumbas na kumwambia,
"Kayumbas hebu mwambie baba yako habari nzuri naye afahamu."
"Enhee, uuu.. umee.. umeokota aaa..aalmasi nini?" Anaingilia kati baba Kayumbas akitaka kumuharakisha Kayumbas kumfahamisha lakini anaonywa na mama Kayumbas.
"Eeeh eeh baba Kayumbas! Utawafundisha watoto kuwaza hela za bahati nasibu. Lazima utoke jasho ndiyo ufanikiwe. Siyo kwa kuokota."
"Natania tu. Ka si.. si.. si uuu..uumemuuuelewa mama yako?" Baba Kayumbas anajaribu kuufuta usemi wake na kutaka kujua kama Kayumbas aliyekuwa akimuita 'Ka' kwa ajili ya kumrahisishia maongezi, alikuwa ameielewa falsafa ya mama yake ambapo Kayumbas akamjibu,
"Ndiyo baba nimemuelewa."
"Enhee, ni..ni..ambie hizo ha... ha..habari."
"Nimefaulu mtihani wa taifa wa daratha la nne."
"Enheee, heee ni..ni..nilikwambia mimi mmm..mm..ma Ka. Anasimama kidogo na kwa sauti iliyojaa msisitizo anasema, "Mtoto tumepata." Kimya kingine cha sekunde kadhaa na kisha anamalizia, "Ho..ho..hongera sana mmm..m..mwanangu, yani ho..ho..hongera sana."
"Athante baba."Anaitikia Kayumbas na kisha baba yake anauliza,
"Eee enhee, kwa hiyo uuu..uu..umekuwa wa ngapi shuleni?"

[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi