"Eee enhee, kwa
hiyo uuu..uu..umekuwa wa ngapi shuleni?"
"Nimekuwa wa thaba."
"Iii..itabidi ni..ni..nikupe
zawadi. Iii..iii..ikifika Jumaa..mosi
ni..ni..nikumbushe ni..ni..nikupe hela uu..uu..uende na mmm..mmama
mm..m..mkanunue nguo."
"Na mimi
baba."....... "Na mimiiii, nataka nguo mpya."
Wadogo zake Kayumbas:
Mjanja na Majaliwa wanaingilia na mama yake huku akinyanyuka kwenda kumuwekea
chakula mumewe anasema kiutani.
"Mwenzangu kazi
unayo. Wao wanataka tu nguo mpya wakati hawajui mwenzao hajapata hivi hivi tu,
amefanya kazi kubwa."
Mara Mjanja anaanza
kulia na baba mtu anamnyanyua na kuanza kumbembeleza akisema,
"Wote humu mmm..mmm..mtapata
nguo mmmpya. Hata mm..mimi ha..ha..hata mm..mmama yenu a..a..atapata nguo mmmpya.
Uu..uu..umesikia Mja? Au..au..au mmmama yeye aaa..a..asipate?"
Mjanja anaitikia kwa
kichwa na kuwafanya wote pale ndani wacheke wakati huo mama Kayumbas akimaliza
kuweka chakula kwa ajili ya baba Kayumbas na kummiminia maji ili anawe. Kabla
ya kuanza kula, anauliza
"Mm..mm..mmama Ka,
ndo uu..uu..umemchinjia mmmwanao kuku?"
"Ndiyo baba Kayumbas.
Nimeona nimpongeze mwanangu."
"Eeee vi..zuri."
Baba Kayumbas anawageukia wadogo zake Kayumbas na kuwauliza,
"Jenni, Mmmja na
Mmmawa si mmm..mm..mnamuona ka..ka yenu aaa...aa..aanavyojitahidi? Na..na..na
nyie mmm..mm..mtafaulu mmkifika darasa la n..ne?"
"Mimi nitafaulu
baba." "Hata mimi mwenyewe nitafaulu." Anajibu Jennifer
akifuatiwa na Majaliwa.
"Yasije kuwa ni
maneno tu wana oko. Ndiyo msome kama kaka yenu." Mama yao anakuwa ameingilia
mama yao.
"Na mimi nataka
niende shule." Anapaza sauti Mjanja ili aweze kusikika zaidi ya dada na
kaka zake waliokuwa wakijimjibu baba yao.
"Utaenda tu
mwanangu, Majaliwa akiingia tu darasa la kwanza na wewe unaanza
chekechea." Anajibu mama Kayumbas.
"Eeeh eeeh naanza
shule." Anashangilia Mjanja asijali kama ni usiku na hapo baba yake anamkemea,
"Aaa..a..acha
kelele sasa, uu..uuusiku huu."
Wanaendelea na
mazungumzo ya kawaida mpaka wanapokwenda kulala.
Kesho yake asubuhi
wanapoamka, pilika pilika zinaanza kama kawaida. Mapema asubuhi Kayumbas na Jennifer
wanakwenda kuchota maji kwenye nyumba moja iliyopo mtaa wa pili wa ule wakaao.
Wanawahi mapema sana na kuanza kugonga geti ili wafunguliwe maji.
"Na nyie? Kila
siku mnakuja asubuhi asubuhi ka wanga? Mnatusumbua bwana, sisi bado tumelala."
Kayumbas na Jennifer wanakaa kimya kwani haikuwa mara ya kwanza kuambiwa hivyo
na watu wa nyumba hiyo. Wanamsikiliza anavyolalamika mtu huyo huku
akiwafungulia geti.
"Kwa nini msiwe
mnakuja wakati jua limeshachomoza?" Anauliza mfanyakazi wa ndani wa nyumba
hiyo aliyekuwa mwanamke mnene mnene wa miaka inayocheza karibu na ishirini
hivi.
"Si kunakuwa na
foleni muda huo?" Anajibu Jennifer kwa kujiamini.
"Si mtasubiria,
mbona wenzenu wanasubiria?" Anajibu akionesha kukerwa na swali la Jennifer.
"Tutachelewa shule
thatha." Anajibu Kayumbas huku akilisogelea bomba na kuweka ndoo yake kwa
ajili ya kujaza maji.
"Basi muwe
mnachota usiku mkalala na maji."
"Aah sisi tumezoea
kuchota asubuhi, usiku tunakuwa tumechoka na kazi zingine." Anajibu
Jennifer.
"Aya shauri yenu.
Siku mtajikuta mkichoma mahindi hapa mpaka saa moja ndo mkafunguliwa."
Hawasemi neno tena na
kuchota maji. Wanarudia tena na kisha Kayumbas kumalizia ndoo yake ya tatu
wakati Jennifer akiishia kuchota ndoo mbili.
Baada ya kumaliza
kuchota maji, Jennifer anafagia ndani na nje ya nyumba wakati Kayumbas
akikimbia kwa baiskeli kwenda kununua mboga mboga kwa ajili ya biashara ya mama
yake kutoka kwenye mashamba madogo madogo mbali kidogo kutoka wanapoishi ambapo
magari hayawezi kufika. Mama yao anaosha vyombo na kuanza kupika chapati kwa
ajili ya kuziuza.
Jennifer anapomaliza,
anapika chai kabisa na hata Kayumbas anaporudi, wanafunzi hao watatu yaani Kayumbas,
Jennifer na Majaliwa wanaoga kwa ajili ya kwenda shule. Wanakunywa chai na
wanapokuwa tayari, mama yao anawapa Kayumbas na Jennifer nauli na shilingi mia
kila mmoja kwa ajili ya kutumia huku akimpa Majaliwa shilingi hamsini kwa ajili
hiyo hiyo ya kutumia.
Bila ya kusahau fagio
zao isipokuwa kwa Majaliwa, wanamuaga mama yao na kwenda zao shule. Jenifer anakwenda
kupanda gari kituo cha nyumbani kwao, umbali wa kama mita mia mbili hivi lakini
Kayumbas inabidi ampeleke Majaliwa shule kwanza umbali wa kama mita mia tatu
hivi na ndipo apande gari la kwenda shuleni kwake.
[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]
tupostie inavoendelea
ReplyDeletesamahan nilikuwa nimezongwa kidogo, sasa endelea nayo!
Delete