Thursday, August 13, 2015

Hatua za kufuata katika kuchekesha… Njia maridadi ya kutoa kichekesho

Kabla sijazungumzia hatua za kufuata katika kuchekesha, ningependa kugusia hatua ambazo mtu hufuata wakati wa kucheka. Si mara zote hatua hizi hufuatwa zote na si mara zote hatua hizi hufuatwa kimpangilio. Lakini, izingatiwe kwamba zaidi ya asilimia themanini wakati wa kucheka, hatua hizi hufuatwa.
Mara nyingi katika kucheka, huanza kwa matayarisho au utayari wa kucheka. Ni mara chache sana mtu hucheka bila ya kuwa ametayarishwa ingawa vichekesho visivyopitia mtu kutayarishwa ndivyo husababisha kuchekesha zaidi. Kwa kupitia utayari huo, kucheka kunaweza kutokea kwa namna mbili. Kwanza na mara nyingi ni pale mtu anapotayarishwa naye kujua tukio linalofuata linahusisha kucheka. Mfano, watu wengi hupenda kusema, “Ngoja, nikuchekeshe bwana…” au misemo inayoendana na huo. Mfano mwingine ni pale mtu anaposoma kichekesho kwenye simu yake na kuanza kucheka akijua unamuona. Kisha mtu huyo bila ya kupoteza muda, pengine bado akicheka anamuonesha kichekesho hicho mtu mwingine. Kwa namna hii, mtu anakuwa ametayarishwa kwa kucheka wazi wazi. Pili, ni pale mtu anapotayarishwa bila ya kuwa na uhakika kama kauli zitahusisha kuchekesha au hapana. Utayarishaji huu wa pili, ndio wenye nguvu zaidi katika kuchekesha. Mtu huhisi kitu fulani cha kuchekesha kwamba kitatokea bila ya kuwa na uhakika Kisha kitu hicho kinapokuwa kweli, ndipo mtu anajikuta katika hali ya kucheka.
Hatua ya pili katika kucheka ni kusikia au kuona ama kusoma kichekesho. Hapa mtu husikia kauli au mfuatano wa sentensi wenye lengo la kuchekesha. Sina haja ya kuelezea maana ya kichekesho au namna vichekesho vilivyo kwani naamini hata mtoto atakayezaliwa kesho anajua maana ya kichekesho.
Hatua ya tatu katika kucheka ni mtu kukihusisha kichekesho na sehemu ya ubongo wake itakayokitafakari kichekesho kile na kujenga uhusiano na picha fulani kichwani mwake. Mchekeshwaji hujaribu kutafuta uhusiano baina ya kichekesho na matukio yaliyowahi kutokea huko nyuma ama matukio aliyowahi kuyasikia na kuyajengea picha kichwani au kujenga picha fulani kichwani akitumia wahusika na mandhari anayoitambua vema. Yaani kujaribu kupata picha mtu anayemjua au mahali anapopajua panatokea kilichoelezwa kwenye kichekesho hicho.
Hatua ya mwisho katika kucheka, yaani kucheka kwenyewe kunategemea sana na hatua ya nyuma yake. Kama mtu ataweza kujenga picha fulani au kukumbuka picha fulani inayoendana na kichekesho kwa kutumia wahusika na mandhari aijuayo vema, basi mtu huyu lazima atacheka.

Hatua za kufuata katika kuchekesha…
Baada ya kuelewa hatua zinazofuatwa mara nyingi katika kucheka, ni vema kuzingatia hatua hizo katika kuchekesha pia. Yaani ili kujihakikishia kwamba kichekesho chako hakipotei bure, ni vizuri kama utafuata hatua za kucheka ili kuchekesha.
Katika kumtayarisha mtu kwa kucheka, ni busara kuanza kufanyia mazoezi kumtayarisha mtu bila kumuweka wazi kwamba una nia ya kuchekesha. Baadhi ya watu husema kwamba Tanzania hatuna watu wenye uwezo wa kuchekesha lakini nikitathmini, naona kwamba kinachokosekana ni utayari wa watu kucheka na pengine ni kufeli katika kuwatayarisha watu kucheka. Njia nzuri ya kutayarisha watu kucheka ni kuruka hatua ya kutoa kichekesho na kumpa mlengwa muda wa kutengeneza picha kuhusu maelezo. Yaani kumfanya mtu aende hatua ya tatu hapo juu kabla ya kupita ya pili na kisha kuendelea na kichekesho. Ndiyo, wachekeshaji wengi hasa wale wafanyao ana kwa ana mbele za watu, hutumia njia hiyo ya kutayarisha.
Umewahi kusikia mtu akiuliza, “Niseme nisiseme?” na baada ya hapo kauli inayofuata inavunja watu mbavu? Hapo, mtu hufanya watu kujenga picha mbali mbali na kwa namna moja ama nyingine kuweka uwezekano wa kutokea kichekesho. Hivi karibuni, niliona njia hiyo ikitumiwa na Mhe. Mbowe akitoa hotuba baada ya Mhe. Lowassa kuchukua kadi. Baada ya kuongea mengi, alisema
“Katika ujio huu, kuna mtu mmoja ningependa kumshukuru sana.” Akakaa kimya na kuuliza, “Niseme nisiseme?” Bila shaka alijua alichokuwa akikifanya kwani baada ya kuambiwa aseme(jambo lililokuwa halihitaji kuuliza), Mhe. Mbowe akasema anamshukuru Mhe. Rais na kuweza kuangusha vicheko kwa wanaukawa.
Ukimaliza kumtayarisha mlengwa kwa kucheka, kinachofuata ni kutoa kichekesho kwa namna inayotoa muda mtu kuhusisha kichekesho na ile picha aliyoijenga kichwani. Yaani usikimbilie kusema kichekesho chako mwanzo mpaka mwisho bila kuwa na vituo vya kumpa mtu muda wa kubashiri mwisho wa maelezo yako kabla hujamaliza.
Kimsingi hizo ndizo hatua za kufuata katika kuchekesha. Si nyingi lakini umakini na mazoezi vinahitajika kabla ya vitu uwezo huo wa kuchekesha kukaa kwenye damu.
Katika nakala ijayo, tutaangalia namna ya kuvitumia vichekesho ulivyoviona kwa ajili ya kuchekesha. Hii ni changamoto kwa wengi lakini uvumbuzi unakuja hapa.


No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi