Sababu za watu kucheka...
Furaha ni moja ya vitu
vichache na muhimu ambavyo watu wote wanaweza kumiliki bila ya kugombania
vyanzo vyake. Watu wote wanaweza kuwa na furaha hata kama kutakuwa na tofauti
nyingi kama za kipato, jinsia, rangi ya ngozi, uwezo wa viungo vya mwili na
vitu vingine.
Kwa vile kucheka ni
njia namba moja ya kuonesha kuwa na furaha, haina budi watu kuwa na utayari wa
kucheka wanapokuwa na furaha. Pamoja na utayari huo, lazima kuwe na chanzo cha
mtu kucheka. Chanzo hicho mara nyingi ni mtu kuchekesha kwa maandishi au
matamshi au maigizo. Kitu ambacho wengi wanakosea nacho nimekigusia katika
nakala zangu za kucheka ni watu kudhania kwamba swala la mtu kucheka ni matokeo
ya uzuri au kueleweka kwa kichekesho pekee.
Kila mtu amezaliwa
akiwa na uwezo wa kuchekesha lakini wengi hucheka mara nyingi kuliko
kuwawezesha wengine kucheka. Mfululizo wa nakala hizi unakusudia kukupa uwezo
wa kuchekesha kufuatia sababu za watu kucheka hata katika mazingira yasiyokuwa
na utayari wa watu kucheka au kupokea kichekesho. Kama tulivyoona hapo awali
kwamba kucheka si matokeo ya kichekesho pekee, basi ili kuweza kuchekesha haina
budi kuzingatia sababu kuu zinazomwezesha mtu kucheka. Baada ya kuona sababu
hizo, katika nakala zijazo tutaanza kuona ni kwa jinsi gani tunaweza kuwa
wachekeshaji asilia, yaani wale wa wakati wote bila kutegemea kuwa na
kichekesho kizuri akilini.
Sababu ambayo wataalamu
wengi wa kisayansi wanaamini ya kuwa namba moja ya mtu kucheka ni kwamba watu
hucheka ili kutengeneza mahusiano katika jamii. Ni ishara itumiwayo kumualika
mtu kuanzisha mahusiano na pia katika kuendeleza mahusiano. Hii hudhihirika
pawapo na vichekesho bubu, yaani watu wawili wanaweza kuangaliana tu na mmoja
kuanza kumchekea mwenzake. Hiyo hasa hutokea kwa jinsia mbili tofauti.
Kuchekesha kwa kutumia njia hii, ipo nje ya malengo ya blogu.
Sababu nyingine
inayoweza kushika namba mbili ni kucheka baada ya kuwa na uelewa unaofanana na
mtu mwingine. Kucheka kwa namna hii, hakutegemei sana uzuri wa kichekesho. Watu
wawili au zaidi wanapoona tukio fulani linalofanana na tukio jingine lililowahi
kutokea, basi huangaliana walionapo tukio hilo la sasa na kisha kucheka baada
ya kuhisi kwamba wote wamekumbuka tukio hilo la nyuma. Kwa kumuelewa vizuri
mlengwa wa kuchekesha kwako, unaweza kuitumia njia hii.
Sababu nyingine ya kucheka
ni kichekesho chenyewe. Hapa sina haja ya kuelezea sana kwa sasa kwani kila mtu
anaelewa kwamba usomapo au kusikia au kuona kichekesho fulani basi mtu hujikuta
akicheka. Lakini mimi bado najiuliza swali moja, ‘Je, mtu ukiwa peke yako na
ukiwa na mtu mwingine jirani, kwa nini inakuwa rahisi kucheka uwapo na mtu
kuliko ukiwa mwenyewe?’ Katika nakala zijazo, nitajikita katika kipengele hiki
ambacho wengi wanakichukulia kama mzizi wa kuchekesha.
Sababu nyingine kubwa
ambayo mara zote hufanya watu kucheka, ni kutokufikirika kwa jambo
linalofanyika. Lugha inaweza kuwa ngumu lakini nazungumzia pale watu
wanapocheka na mmoja kusema, ‘Dah, sijui huyu jamaa alikuwa anafikiria nini.’
Au ‘Duh, sijui hawa watu huwa wanafikiria nini.’ Sifa za jambo hilo ni
kuwezekana kufanyika lakini watu kikawaida huwa hawalifanyi. Hii ni njia ya
uhakika ya kuchekesha ambayo nitaielezea katika nakala zijazo.
Nakala hii inakuwa
ndefu na sasa nifupishe sababu mbili za mwisho zilizobaki zinazomfanya mtu
acheke lakini haziwezi kutumika kuchekesha. Sababu hizi ndiyo hasa pale
tunasema kujichekesha. Moja ni mtu kucheka kufuatia kukosa kile alichokuwa
akikitarajia. Kwa mfano mtu aulizwapo swali gumu au aonapo dalili za kushindwa
anaweza kucheka bila ya kuwepo kichekesho, kicheko chenye chembe chembe za
kujibeza. Na mwisho ni mtu kucheka ama kujichekesha kuficha hisia mbaya
alizokuwa nazo. Mtu anaweza kucheka atokewapo na jambo baya kama vile kutukanwa
na mwenzake ili kuficha hisia za kukasirika kwake. Njia hizi mbili za mwisho ni
ngumu kuzitumia katika kuchekesha.
Katika nakala ijayo
katika nakala hizi za kuchekesha, tutaona umuhimu wa kujua kuchekesha..
No comments:
Post a Comment