Kuchekesha bila
kukariri vichekesho haimaanishi kuwa na uwezo wa kutunga vichekesho vipya au
kuvibadilisha vichekesho vilivyopo. Ninachojaribu kumaanisha kwa umuhimu wa
kujua kuchekesha bila kukariri vichekesho ni sababu za kuchekesha bila ya
kutumia vichekesho(kifungu cha kauli zenye lengo la kuchekesha.)
Miaka mingi iliyopita, nikiwa
mtu ninayejali mambo ya muhimu peke yake, sikuona umuhimu wa kuchekesha wala
kucheka vichekesho vya watu. Sisemi maisha yalikuwa mabaya au magumu lakini
hali ya sasa ni nzuri zaidi kuliko huko nyuma. Muda ulivyokuwa ukienda mbele
nilianza kuona umuhimu wa kujua kuchekesha, acha ile mara moja mara mbili
ambayo mtu yeyote anaweza kuchekesha. Nilitamani kuwa na uwezo wa kuchekesha
kwa haraka zaidi na mazingira magumu zaidi. Unajua nilichokifanya?
Nilianza kutembelea
mitandao mbali mbali inayoandika vichekesho na kuanza kuvikariri vichekesho
hivyo. Ingawa vichekesho hivyo vilikuwa kwa lugha ya kiingereza, niliweza
kuvibadilisha na kuvisimulia kwa Kiswahili kwa namna ambayo ilichekesha. Kadiri
siku zilivyokwenda nami nikawa nikitafuta vichekesho hivyo kwa udi na uvumba
ili wale waliouona uwezo wangu wa kuchekesha wasiache kunisikia nikichekesha.
Halikuwa jambo baya lakini vichekesho hivyo vikawa kama vikijirudia rudia na
kuniboa. Hapo ndipo nikaona umuhimu wa kujua kuchekesha bila kukariri
vichekesho.
Umuhimu hasa ni kuwa na
uwezo wa kuchekesha muda wote na mahali popote. Lakini bado kuna haja ya
kuzungumzia umuhimu wa kuchekesha kwa ujumla wake. Katika hali ya kawaida,
faida kubwa ya kuchekesha ni kujenga na/au kuimarisha mahusiano baina ya watu.
Ipo wazi kwamba watu wanaochekesha huwa na mahusiano na watu wengi zaidi kuliko
wale wasiochekesha lakini ikumbukwe pia kuwa kuchekesha kila wakati huweza
kufanya watu wakutoe maana, yaani uonekane mtu asiyeweza kuwa makini. Kama ni
mfanyakazi, kumchekesha bosi wako kutaimarisha uhusiano wako na bosi huyo na
unajuaje faida ya kuwa karibu zaidi na bosi wako kuliko wafanyakazi wengine?
Umuhimu mwingine wa
kuchekesha ni kutumiwa kama ajira. Mifano hai ipo kwa wale wenye vipindi vya
kuchekesha na kila stesheni, ina vipindi hivyo. Naomba nisihi kwamba kuchekesha
siyo tu kutakupatia ajira ya kuchekesha, bali ajira nyingi zinazohusisha
kuhudumia watu wengi basi kuchekesha kwako, kutakuongezea uwezekano wa wewe
kupata ajira. Kwani hujawahi kusikia watu wakati wakitafuta mwongozaji wa
sherehe wakisema, “Wee? Kuna MC huyo anaitwa Kafupi, yaani balaa kwa
kuchekesha. Tumchukue huyo huyo.” Pia hujakutana na wagonjwa wanaompendelea
daktari fulani kwa sababu anaongea nao vizuri? Anawachekesha?
Nimeanza na hali ya
kawaida, nikafuata yenye umuhimu kidogo na sasa nizungumzie umuhimu wa
kuchekesha katika hali ambayo watu wengi hushindwa kufikiria umuhimu wa kuchekesha
katika mazingira hayo. Hapa ndipo hasa penye umuhimu wa kuchekesha bila ya
kukariri vichekesho. Nazungumzia kuchekesha kama njia ya kukwepa hali tata
upande wako. Inaweza kuwa kukwepa swali gumu kwenye mahojiano, kuinua au
kubadili mkondo wa ushindi kwenye majibizano na hata kuficha ubaya unaotaka
kujitokeza.
Pata picha unakwenda
kwenye masaili(mahojiano) ya kazi na umeme umekatika siku hiyo. Ukaenda na shati
lililojikunja sana ukiiamini elimu na ujuzi wako kuliko umaridadi wako lakini
kati kati ya intavyu, mmoja wa wanaokuhoji akakuuliza, “Kwa nini umevaa shati
lililojikunja sana wakati unajua unakwenda kwenye intavyu?”
Katika hali ya kawaida
mtu anaweza kujaribu kutoa sababu nyingi, ‘umeme umekatika, nimeibiwa shati
langu nililotayarisha, nje tu ya ofisi nimemwagiwa juisi hivyo hili siyo
langu.. n.k) ambazo zinaweza kuzua maswali mengine na mwisho wa siku kuonekana
mtu ambaye hukujiandaa mapema au kwa kiingereza naomba niseme,
‘careless.’(keyales). Kwa mimi ningejibu au ningeshauri mtu yeyote ili kuondoa
umakini wa wale wanaokuuliza katika jambo hilo kwa namna inayofanana na jibu
hili.
“Ooh, huu ni utamaduni
kwetu. Bibi yangu mzaa babu aliniambia nikitaka kufanikiwa kwenye intavyu kama
hizi, nisipige pasi nguo.” Kama bahati mbaya kuna mdudu kwenye nguo na umeulizwa,
unaweza sema, “Ooh, kuna mtu ananitakia kila la kheri kutoka kijijini kwetu.”
Kuna kipindi nilikuwa
katika masaili ya kupewa ufadhili wa masomo nao ungetegemea uwezo wangu wa
kufaulu. Matokeo yangu ya mtihani wa Taifa yalikuwa mazuri lakini mfadhili
hakuamini mara moja na katika kutokuamini kwake akauliza, “Lakini nasikia
shuleni kwenu wasimamizi wa necta huwa wanalipwa.”
Nadhani unaweza kujua
kwamba kukataa kungeleta maswali zaidi na kukubali kungeashiria nisiaminiwe kwa
matokeo tu ya necta. Bila ya kutetereka nilimjibu,
“Yah, ofkoz huwa
wanalipwa.” Nikavuta muda kidogo na kumalizia, “Na Necta (yaani baraza la
mitihani) lakini.” Wote katika chumba walicheka na kutohoji tena kuhusu maswala
hayo.
Sasa tumeona umuhimu wa
kujua kuchekesha bila ya kukariri vichekesho, katika nakala ijayo tutaona hatua
zinazofuatwa katika kucheka na hivyo hatua za kufuata katika kuchekesha…
No comments:
Post a Comment