Watanzania ni wakarimu
sana, kila mtu analisifia hilo. Ni jambo la ukweli na la kupewa sifa. Hata
mtoto mdogo wa kitanzania anatambua ya kuwa jambo lolote linaloonesha kuwa la
kutokufurahisha linapomtokea mtu, basi jambo zuri na la kwanza kabla ya yote ni
kumpatia pole mtu aliyefikwa na janga hilo. Matokeo yake ni kwamba tumekuwa
kama mashine, yaani ukiona mtu anasikitika basi wewe ni … ‘pole…’ na imepita
hiyo.
Sisemi tuache kusema
pole kwani vipo vingi vya kurekebisha na inategemea na mtu. Wapo baadhi ya watu
ambao kiukweli hupenda kusikia wakiambiwa pole na hivyo kusema pole kwao,
hufanya kazi bila matatizo. Lakini linapotokea tatizo kubwa kama ugonjwa au msiba,
basi lazima kuwa makini katika kutoa pole. Mfano tuchukulie swala la msiba, mtu
wa kwanza kasema pole akaeleweka. Akaenda wa pili naye akaeleweka. Wa tatu, nne
na kuendelea. Wewe unasikia kutoka kwa mtu na kwenda kutoa pole kama ya
ishirini hivi. Je, unadhani kufika pale na kusema maneno yale yale, “Nasikia umefiwa
na [ndugu] yako. Dah, jamani hivi ameondoka kweli, pole sana.” Kutamfanya mfiwa
akumbuke kwamba uliguswa? Au unajisikiaje unaporudi kutoka kwenye mazishi
mkoani halafu unamwambia mtu kuwa ulikwenda kuzika, halafu unachosikia ni,
“Pole ndugu yangu.”? Ongeza thamani ya utu wako kwa kutoa pole kistaarabu.
Mtu aliyestaarabika,
hudadisi tatizo na ukubwa wake kabla ya kutoa pole. Pole ya kistaarabu pia
huambatana na maneno ya kuisindikiza yaani huvalishwa nguo. Lakini pia katika
hali ya kawaida, inaweza kukulazimu kutoa pole zaidi ya moja kama mtu apokeaye
pole hiyo atakuwa akisimulia mfuatano wa matatizo au matukio yanayokulazimu
kumuonea huruma. La kukumbuka ni kwamba, hata ukitoa pole mia kwa mtu mmoja
katika muda mmoja, ni vema pole hizo zikawa zikitofautiana usemaji au utolewaji
wake.
Ushauri wangu: Jifunze
kutumia kauli ya, “Pole kwa …” ukimalizia na jambo linalokufanya umuonee huruma
huyo mtu. Kisha, jifunze kutokukimbilia kusema pole kwani muda mwingi
inamkatisha tamaa yule anayekusimulia majanga yake. Kwa kujifunza taratibu
unaweza kugundua ni muda upi muafaka wa kutoa pole wakati mtu akikusimulia
matatizo yake. Lakini kama unayajua matatizo kabla ya kuambiwa na huyo mtu,
pengine umesikia kutoka kwa watu, ni vema kuanza na ‘Pole kwa…’ kisha kuanza
kudadisi ukubwa wa tatizo na kama suluhisho limepatikana au la. Lakini katika
yote, usisahau kutoa pole mara ujuapo ukubwa wa tatizo hata kama suluhisho
limeshapatikana.
Katika nakala ijayo
katika mfululizo wa nakala hizi za Lugha ya Maneno tutaangalia Namna ya kupokea
pole kwani Kusikia ukiambiwa pole siyo kazi, kazi kuipokea pole unayopewa.
No comments:
Post a Comment