Friday, July 31, 2015

Damu Ya Ukoo Wangu: Sehemu ya 3



Roho ya kishetani ilikuwa ikizidi kuniingia akilini na tayari nilishakata shauri, nikashika njia kwa haraka bila hata ya kugeuka nyuma kutoka nje ya hospitali hiyo nikijificha nisionwe na ndugu na jamaa pale hospitali. Nilipanda gari hadi kariakoo ambako nikachukua gari ya ubungo na kushukia magomeni Kagera ambako ndiyo nyumbani. Niliingia ndani na kumkuta mtoto wangu Matata akiwa amejilaza kwenye malu malu akichora chora kwenye gazeti. Aliponiona tu akaniamkia,
“Shikamoo ba mkubwa.”
Japo alikuwa ni mwanangu wa damu, alikuwa amefanana sana na Shukuru na kutokana na baadhi ya mambo yaliyotokea huko nyuma, mtoto huyu alijua Shukuru ndiyo baba yake. Na wote kasoro Shukuru na mke wangu tulifanywa tudhanie hivyo.
“Marahaba. Njoo ulale huku muda umefika wa kulala mchana.”
Nilijibu kwa sauti ya kawaida nikijitahidi kuficha hasira zilizokuwa zimetokana na hali mbaya ya mke wangu na kwamba zilisababishwa na mtoto huyo Matata. Mtoto ambaye nilichukua muda kuamini ni damu yangu naye akawa akihitajika dunia nyingine. Nilijitahidi kumzuia abaki dunia yetu ya kawaida lakini maji yalikuwa yamenifikia shingoni, nilishindwa kuruhusu kupoteza kila kitu kwa ajili yake.
Mtoto huyo alionesha kutokupendezewa na swala la kulala muda ule lakini kwa vile alikuwa akiniogopa, alishindwa kubisha na kunifuata mpaka chumbani. Hiyo ilikuwa muhimu ili mimi kuweza kukamilisha makubaliano na nguvu ambayo ilikuwa ikimuua mke wangu kwa kuinyima almasi yake. Nguvu hiyo ndiyo ilikuwa mpinzani wangu na muda wa wote kushinda ulikuwa umefika.
Sehemu ya moyo wangu ilikuwa ikinikataza lakini sehemu iliyobaki ilinionesha nuru na mafanikio ya mimi kuweka makubaliano na nguvu hiyo. Nililala chali kitandani nikijihisi mtu katili na asiyefaa kwenye jamii. Uwoga ulikuwa ukiongezeka ndani yangu na kunifanya nianze kumuonea huruma mtoto huyo. Ule upande wa pili nao ulikuwa ukiniambia nisipofanya makubaliano basi nitakuwa sijawatendea haki watu wengi.
‘Lakini kwa nini ruhusa lazima itoke kwangu?’
‘Labda kwa vile mimi ndiyo mtoto wa kwanza wa familia yetu.’
‘Sasa ndiyo nimtoe kafara hata mtoto wa Shukuru?’
‘Siyo kafara, hiyo ni sadaka kwa Shukuru na msaada kwa Matata. Huku atateseka tu bora akawaongoze huko wamtakapo’
Maswali yalinifululiza kichwani na kujaribu kujijibu mwenyewe. Nilipofikia hapo, nikajikuta nikipata wazo ambalo nilijua lingeweza kumaliza maamuzi yangu. Nilimgeukia Matata aliyekuwa amefumba macho kujaribu kutafuta usingizi.
“Matata mwanangu, najua wewe bado mdogo kuelewa hivi vitu lakini kama ni kweli basi utanielewa. Nimejitahidi kufanya kile ambacho ndugu yeyote angekifanya lakini naogopa ninaweza nikawa kweli nikikosea. Naomba unioneshe kama walichokisema kuhusu wewe ni ukweli au walidanganya.”
Nilipomaliza kuongea maneno hayo juu ya sikio la kulia la Matata, nilinyanyuka na kwenda nje ambapo nilichukua kijiti na kuingia nacho chumbani. Kisha nikachukua peni na karatasi na kuviweka vitu vyote pamoja, peni na kijiti vikiwa juu ya karatasi.
“Matata, chagua kitu cha kuchorea kwenye karatasi.”
Nilimuamsha mtoto huyo na kumuomba hivyo huku nikimuashiria kwa mikono achague kati ya peni na kijiti. Matata alianza kufurahi akichukua kijiti na kukishikilia kwa nguvu mkononi.
Macho yalinitoka kama mjusi aliyebanwa na mlango nisiamini nilichokiona. Hatimaye niliweza kuelewa chanzo cha matatizo kwani maelezo ya yule mchawi yalikuwa yakijihakikisha ukweli wake sasa. Matata tayari alishafumba macho namoyo wangu tayari ulishafanya maamuzi.

 [Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi