Friday, July 24, 2015

Matayarisho ya mwisho...

Kwa nini uhitaji au kwa nini usihitaji kubobea katika lugha ya maneno…
Nianze kwa kukumbushia kuwa lugha ya maneno inadhamiria kukupa ujuzi na uwezo wa kunasa baadhi ya maneno mtu asemayo kupitia kauli zake yanayobeba dhamira halisi aliyo nayo. Pia itakusaidia kuweza kufikisha dhamira yako namna unavyotaka bila ya kuwepo kwa makundi au tafakari tofauti za kauli zako.
Si kwamba bila kuwa na ujuzi sahihi wa lugha ya maneno basi hutaweza kuwaelewa watu au watu kutokuzielewa kauli zako, lakini hii inalenga zaidi kwenye dhamira ya ndani au tafakari iliyo sahihi zaidi. Si wote watakaohitaji ujuzi huu nawe usijisikie vibaya utakapoona kuwa haina umuhimu kuwa nao. Kwa wewe unayeona umuhimu, ninakukaribisha sana katika safari hii na nikuhakikishie kuwa utaanza kuona mabadiliko baada ya nakala chache tu. Ujuzi ni kama utajiri, kama watu wote tukiwa matajiri basi neno hilo ‘utajiri’ halitakuwa na maana. Ndivyo ilivyo kwa upande wa ujuzi, kama watu wote tukijua kwa kiwango sawa, basi ujuzi wetu hautakuwa na maana. Chaguo ni lako kupenda kujua au kuchukia kujua.

Je, uko tayari kujua?
Vuta na kushusha pumzi, fumba macho na tafakari kwa muda. Kumbuka kuwa tendo moja linakuwa na matokeo tofauti kwa watu tofauti. Pata picha ametokea kichaa aliyekonda sana na kukuchanja kwa kutumia kiwembe ambacho kinaonekana wazi kimeshatumika. Je, katika swala la Ukimwi hofu yako kubwa itatokana na tafakari ipi kati ya hizi?
‘Bora hata nisiende kupima, nisije kujipa mawazo kama nitakuta ninao.’
‘Bora nikapime ili nijijue afya yangu, kuliko kuishi kwa mawazo siku zote kwa sababu sijui kama ninao au sina.’
Hivyo ndivyo watu wanavyotofautiana na hakuna namna ya kumbadilisha mtu mawazo yake kutoka upande mmoja kwenda mwingine. Kama wewe una mawazo kama ya mwanzo katika mfano huo, basi nikutahadharishe kuwa na umakini zaidi utakapozijaribu njia hizi. Pale unapokata shauri kuanza kuzitumia njia hizi, basi ni kheri kujiamini na kuamini kile utakachokinasa kutoka katika maneno yatakayotumiwa. Changamoto kubwa iliyopo katika matumizi ya lugha ya maneno ni watu kupingana na ukweli utokanao na maneno wanayoyatumia.
Msanii mmoja katika wimbo wake aliokuwa akiwahasa vijana wa kiume katika mahusiano, alitahadharisha akisema, ‘gusa unase…’ Siku moja alipohojiwa maana ya maneno hayo akakiri ya kuwa maana halisi aliyokuwa ameifikiria yeye mwenyewe, iligundulika kuwa dhaifu kwa mashabiki wake ambao walimpa maana inayofaa kutokana na maneno yale naye akakubaliana nao.
Maneno na vitu vingine vidogo vidogo hubeba dhamira halisi wakati kauli kwa ujumla, hubeba ujumbe ambao mtu anapenda ukufikie. Katika mojawapo ya nakala zijazo, nitakuelezea mbinu mojawapo isemayo, ‘Sikiliza wasichokisema, kila mtu husikia wanachokisema.’
Lakini kabla ya kujikita zaidi katika kujua dhamira za watu kupitia nakala za pata ujumbe sahihi, nishauri watu kuanza na nakala za staarabika na staarabisha pamoja na za toa ujumbe sahihi. Katika staarabika na staarabisha, maneno mbali mbali yatumikayo kimazoea au vibaya, yatakuwa yakielezewa matumizi sahihi.

Usikose nakala zinazofuata…
Staarabika na Staarabisha: Kusema pole siyo kazi, kazi kutoa pole… pia Kusikia pole si kazi, kazi kuipokea pole.
Toa ujumbe sahihi: Unatoa taarifa au unauliza swali! Hatutaki kusikia taarifa ya swali…

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi