Tuesday, July 21, 2015

Damu Ya Ukoo Wangu: Sehemu ya 2


Maiti ilikuwa ikitolewa wodini kupelekwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti. Taratibu huku hofu ikiwa inanizidi nami nikihisi bora ya kufa kama mke wangu akifa kwa sababu yangu nilijongea kwenye machela hiyo. Nilipoikaribia sikuweza kutembea taratibu tena bali nilijikuta nikipiga hatua mbili za haraka na kuivamia maiti ile nikiifunua sehemu ya kichwani. Japo mikono ya wauguzi ilijitahidi kuwahi kunizuia kutokuifunia maiti hiyo, nilifanikiwa kuona paji la uso pamoja na nywele. Nashukuru Mungu haikuwa maiti ya mke wangu na ahueni niliyoipata ilinifanya nishushe pumzi kwa nguvu na moyo kuhema kama vile mtu aliyekoswa na risasi.
 Bado nikiwa ninahema nilihisi mikono ikinishika karibu na mabega yangu na kunifanya nigeuke nyuma. Shukuru, mama bonge, Jeni pamoja na Tumsifu walikuwa wamesimama nyuma yangu wakinitazama kwa shauku kubwa. Shukuru ambaye ndiye alikuwa amenishika akauliza,
"Ni mwenyewe?"
Nikijitahidi kutabasamu ili kuwatoa shaka, nilitikisa kichwa changu bila ya kutoa neno. Wote waliweza kuona kuwa nimeyaelekeza macho yangu kwa yule daktari ambaye tayari alikuwa akiondoka sasa. Shukuru ambaye muda huo alikuwa mbele yangu, aligeuka nyuma na kuanzisha safari ya kumfuata yule daktari. Mimi ndiye nikawa nyuma nikiwafuatia wenzangu taratibu kujipa nafasi ya kuweza kutafakari nini cha kufanya.
Tukiwa tunamuelekea yule daktari, Shukuru akiwa kama hatua tano kumfikia huku mama bonge, Jeni na Tumsifu wakiwa nyuma ya Shukuru kwa kama mita nano na mimi nyuma yao kama hatua nane, nilistushwa na sauti niliyoisikia ndani ya kichwa changu.
'Kuna haja ya wewe kuongea na daktari?'
Nilisimama nikihisi mpinzani wangu alikuwa akijaribu kuongea na mimi japo nilijua asingeweza kuwa yeye. Nilivyosimama sikusikia tena sauti yoyote bali sehemu ya ubongo wangu ilikuwa ikiniambia kuwa kweli hakukuwa na sababu ya kumuona daktari. Baada ya kukubaliana na wazo hilo nikahisi kitu kikiniambia moyoni,
'Mke wako anakufa na wewe umesimama tu kama vile hujui cha kufanya?'
'Usiutese moyo wako, acha moyo wako ukuongoze sasa kwa kuwa ukifuatisha ubongo wako utakuja kuumia sana moyo. Usitake watu wakuone mwema wakati unajitengenezea madonda moyoni, upendo wako upo kwa mkeo na si kwa Matata.'
Roho ya kishetani ilikuwa ikizidi kuniingia akilini na tayari nilishakata shauri, nikashika njia kwa haraka bila hata ya kugeuka nyuma kutoka nje ya hospitali hiyo nikijificha nisionwe na ndugu na jamaa pale hospitali.
Soma nyuma.
 [Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi