Saturday, July 25, 2015

Mambo ya kuzingatia kuhusu kucheka… Cheka panapostahili, kujichekesha sio dili!



Mchango wa Hadhi(Wadhifa) katika kucheka.
Katika nakala iliyopita kwenye mfululizo wa nakala hizi, tuliona jinsi uhusiano na hisia zilivyo na mchango katika kumfanya mtu acheke awapo na watu fulani. Tuliona kwamba mtu anacheka kirahisi awapo na familia yake ama kazini, yaani jinsi uimara wa uhusiano ulivyo au hisia zilizopo ndiyo urahisi wa mtu kucheka ulivyo.
Katika nakala hii tunageukia katika kitu kingine ambacho kina mchango mkubwa katika kumfanya mtu acheke. Wengi tumewahi kulishuhudia hili ingawa kuna uwezekano hatukuliwekea mkazo. Tumeona katika filamu nyingi, pale mkuu au bosi wa kikundi fulani anapotokewa na kitu cha kuchekesha ambacho kinaweza kuwa kikimuaibisha kwa namna moja au nyingine, wale wafuasi hucheka endapo tu mkuu wao ataanzisha au kuruhusu wao kucheka na punde atakaponyamaza, basi nao hufuata.
Rafiki yangu mmoja aliwahi kuniambia kauli moja, ‘Huhitaji kuwa mchekeshaji, ukishakuwa tajiri basi watu karibu yako hujikuta wakicheka tu hata ukiongea pumba.’ Hakuwa akikosea. Ukweli ni kwamba watu wawapo na watu wenye hadhi kubwa zaidi yao, hujikuta katika hali ya kucheka zaidi kuliko wakiwa na watu wa hadhi ya chini yao au hadhi sawa.
Umewahi kuona namna watu waliokaa meza moja katika baa wanavyocheka? Au kikundi cha watu wa ofisi moja wakicheka? Vicheko huongezeka na watu kuwa huru zaidi endapo mkuu au bosi yupo katika kundi hilo. Mchango wa mkuu au bosi huyo katika kuwafanya watu kucheka ni pale atakapotoa kichekesho ambacho anategemea watu wacheke au atakapoanzisha kucheka kichekesho cha mtu mwingine.
Pia hili tunaweza kuliona katika familia zetu na kama tunakumbuka kipindi tukiwa tunasoma. Kichekesho hicho hicho kikitolewa na kaka au dada nyumbani kitachekesha tofauti kama kitatolewa na mama au baba wa familia. Hivyo hivyo ndivyo ilivyo endapo mwalimu atajaribu kutoa kichekesho kwa wanafunzi wake. Hata kama kichekesho kitakuwa cha kawaida sana au hakichekeshi, bado wanafunzi watajikuta wakicheka.
La kuzingatia… Kucheka uwapo na mtu mwenye hadhi zaidi yako, ni jambo linalotakiwa kutokea bila ya kujifikiria. Kumbuka kucheka kunatokea pale tu mtu awapo na furaha, hivyo kuonesha una furaha kuwa pamoja na mtu huyo ni jambo la msingi. Huhitaji kujichekesha, lakini kuweka akilini kwamba mtu uliyekaa naye ana hadhi zaidi yako na hivyo anakutendea wema kukaa na wewe na kujaribu kukupa furaha kwa kukuchekesha, basi utajikuta ukivielewa vichekesho vyake na kucheka bila pingamizi. Pia, unaweza kutazama namna watu wa kundi moja wanavyocheka na kutambua mkuu katika kikundi hicho.
Katika nakala ijayo; Mchango wa matayarisho ya kucheka kabla ya kucheka…  

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi