Tuesday, July 21, 2015

Roho ya Kayumbas: Sehemu ya 2


Mwaka 2006
Majira ya saa nne wakati jua likianza kuchoma maeneo ya Yombo-Buza katika wilaya ya Temeke, Kayumbas anarejea nyumbani kutoka shuleni alipokuwa amekwenda kupata matokeo yake ya mtihani wa Taifa wa darasa la nne. Uso wake umetandwa na furaha na anamkuta mama yake akitwanga kisamvu nje ya nyumba waliyopanga.
Nyumba hiyo iliyojengwa maalumu kwa kupangisha imejificha kutoka barabarani nayo ina vyumba kumi na mbili, vinne vikiwa uwani mwa nyumba kubwa. Imechukua wapangaji wa familia tatu tofauti, akina Kayumbas wakiwa familia mojawapo.
Kwa mbali kidogo kutoka alipo mama yake, yupo mdogo wake aitwaye Mjanja  akipiga mswaki. Huku akishangilia, Kayumbas anamkimbilia mama yake na anapomfikia wanakumbatiana.
"Mana oko, imekuwaje huko?"
"Nimefaulu mama kuingia daratha la tano."
"Mbuta! Mana oko umefaulu kweli unatania?"
"Kweli mama nimefaulu."
Mama Kayumbas anambusu mwanawe huyo kwenye paji la uso akimshika kichwa kwa mikono yote miwili. Anamuachia na kunyoosha mikono juu kumshukuru Mungu.
"Aika Iruwa."
 Mdogo mtu anafanya haraka na kumaliza kupiga mswaki kabla ya kuwakimbilia mama na kaka yake na kuwauliza,
"Kuna nini?"
Kayumbas anamtazama mdogo wake usoni huku akitabasamu kidogo na kisha kumrudia kumuangalia mama yake anayempapasa Mjanja kichwani. Mjanja naye anamkumbatia mama yake kiunoni na kuegemeza kichwa chake kwenye sehemu ya mapaja ya mama yake.
"Kaka yako amefaulu mtihani Mjanja."
Mama Kayumbas anamjibu Mjanja sababu ya furaha yao na hapo hapo Mjanja anamuachia mama yake na kuanza kuruka ruka akishangilia,
"eeeeh eeeh eeh. Kaka amefaulu."
Kayumbas na mama yake wanacheka namna Mjanja anavyoshangilia kana kwamba anafahamu vema maana ya kufaulu. Kisha mama Kayumbas anamwambia mwanawe,
"Mana oko, na imani yangu kwa Iruwa idhihirishwe kupitia kwako. Naamini Iruwa atakuongoza mpaka siku ya mwisho nawe utafaulu vema, nasi wazazi wako tupo kukusaidia kuyafikia malengo yake kwako. Chochote utakachohitaji mana oko, usisite kutuambia. Tutakupatia kila utakacho usije ukaanguka.'
Kayumbas anamjibu mama yake, "Thawa mama nimekuelewa, nitakuja kufaulu tu."
Mama Kayumbas baada ya kuisikia kauli hiyo kutoka kwa mwanawe, anarudi nyuma kidogo na kumuangalia juu mpaka chini kama anayemtathmini na huku akitabasamu, anamsogelea tena na kumuwekea mikono mabegani akisema,
"Mana oko leo nakuchinjia kuku, umenifurahisha sana. Soma mana oko kwa bidii, yani mi nataka mana oko usije ukaishi maisha haya tunayoishi sisi. Kufanikiwa kwako ndiyo mwongozo kwa wadogo zako. Yani, hebu muangalie baba yako, hana hata heshima hapa mtaani unadhani kwa nini?"
Kayumbas anatingisha kichwa chake huku akisema,
"Hamna thifahamu mama."
 Jibu hilo linamfanya mama yake amalizie,
 "Pesa hizo mana oko, baba yako hana pesa za kumpatia heshima hapa. Hivyo mana oko wewe soma uje upate kazi nzuri na uishi maisha mazuri ya kuheshimika."
"Mama, mimi nitathoma hadi nimalize madaratha yote."
"Mana oko, si unajua elimu ni bahari lakini? Sio lazima mpaka uzeekee shuleni, wewe ukifika zako chuo tu inatosha. Utaishi vizuri tu."
"Thawa mama lakini mimi nataka nithome kila kinachothomeka hata nikimaliza chuo kikuu."
"Hapo umenena mana oko, na uwe rafiki na walimu wako ili wakuongoze vizuri, usije ukamchukia mwalimu wako hata akufanye nini."
"Thawa mama."
"Haya nenda uendelee na shughuli zako mana oko."

[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...] 

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi