Sunday, July 19, 2015

Roho ya Kayumbas: Sehemu ya 1

Mwanzo: Utangulizi...


'Triiiii triii triiii triiii triiii...'
    Ni mara ya tatu simu ilikuwa ikiita na kunisumbua usiku huo wa saa tano ambao nilikuwa nimechoka sana kwa kufanya kazi masaa ishirini na nane mfululizo. Nilipanga nilale kama gogo usiku huo lakini simu hii ilikuwa ikininyima raha  bila ya kujua nani aliyekuwa akipiga. Kabla ya kujua nini cha kufanya kuhusu simu hiyo, mwenzangu niliyelala naye akanitingisha, "......" 
    Akaniita jina fulani la kipekee nisilopenda wengine walichukue na kuniambia, "Kuna mtu anasumbua kwenye simu yako."
Sauti hiyo ambayo siku zote napenda kuisikia, ikanifanya ninyooshe mkono wangu na kuichukua simu.
"Haloo mkuu wangu, samahani kwa kuchelewa kupokea." Ni simu ya rafiki yangu mkubwa kwenye maswala ya kikazi. Na nilipoiona tu kuwa ni simu yake nikaelewa ni jambo muhimu.
"Sikutakiwa nikupigie mida hii Kenny, najua utakuwa umepumzika lakini iko hivi bwana, imetokea tena Kenny na nilivyosikia tu sikutaka kuchelewa kukupa taarifa."
"Imetokea tena, nini hiyo? Leo sijaangalia taarifa ya habari."
"Ohooo Kenny? Inawezekanaje, ndiyo kipindi hiki. Kuna habari uliikosa mwaka jana kipindi kama hiki, yametokea tena. Wahi kuangalia kesho asubuhi kabla hujachelewa tena."
Akakata simu na kunifanya nikurupuke pale kitandani. Sikuweza kusubiria asubuhi na hivyo kukimbilia runinga muda huo huo. Nikakuta watu wakihojiwa hojiwa juu ya tukio moja kubwa ambalo sikulijua mara moja. Kati ya waliohojiwa, hawa walikuwa na mambo muhimu sana.
Mama yake: "Wamenipotezea mwanangu hawa. Sijui ni mzimu gani unaoiwinda familia yangu lakini nina uhakika hakufeli hivi hivi. Kuna mtu alichezea akili ya mwanangu lakini yeye mwenyewe hakujua. Mwanangu alisoma kwa shida sana lakini kamwe hakuchoka kusoma. Wote tulitegemea angefaulu kwa alama za juu lakini nashangaa kusikia eti amefeli.... Ndiyo, ameacha barua mbili, moja ya kwangu na nyingine amesema nimpe Mashoto... Aseme nini zaidi ya kujilaumu na kunilaumu, lakini siwezi kusema sana kwa kiasi fulani labda nilichangia."
Mjanja(mdogo wake): "Kaka ametukimbia na tutammis siku zote kwa sababu tulimtegemea aje kuwa baba wa familia. Alikuwa kati ya watu wanaojipigia mstari na kuufuata mstari huo wasijali pembeni kunatokea nini. Nilimpenda sana kaka yangu lakini sijui upande wake... Ndiyo, mimi nilikuwa wa kwanza kuacha shule na kaka alinichukia sana kwa sababu hiyo. Alitaka nisome, nakumbuka alivyokuwa akinipeleka shule utotoni lakini.... Hapana, alikuwa tayari kuanza kufanya kazi zetu hizi zisizohitaji elimu lakini nafikiri ni ile hali ya kuzidharau kazi hizi."
Mwalimu wake: "Sijawahi kufundisha mwanafunzi bora kama yeye. Hata kipindi mimi nasoma sikuwahi kumuona kama yeye. Alikuwa na determination(malengo), alijua nini afanye kufikia malengo yake na kikubwa zaidi, alimpenda kila mmoja. Alitaka anavyofanikiwa yeye basi kila mmoja naye afanikiwe.... Yah, siwezi kuhesabu ni mara ngapi aliwahi kunifuata akitaka nimsaidie ushauri lakini nilichokigundua ni kwamba kulikuwa na ugumu sana kumshauri kinyume na malengo yake. Alijiamini kupita kiasi... Hapana baada ya matokeo kutoka niliongea naye na kumuambia kwamba bado ana nafasi, niliamini kwa moyo wake asingekata tamaa. Nilijitahidi kumpa moyo na kumsifia kwa makubwa ya kukumbukwa aliyowahi kuyafanya lakini hakuwahi kutosheka... Alitaka kila kitu na angepata kama angeendelea kuvumilia kidogo ."
Habisai(Mwanafunzi, rafiki mkubwa): "Alikuwa rafiki yangu mkubwa kuliko wote niliowahi kuwa nao maishani. Alikuwa akimjali kila mtu na hata nilipokuwa nikijaribu kumshauri afuate mambo yake ili afanikiwe zaidi yeye aliendelea kupigania yake na ya wengine.... Hamna, isipokuwa tu kwamba hakuwa mtu wa kushaurika. Kwa nilivyomjua, mtu pekee aliyekuwa na uwezo wa kumshauri akaeleweka alikuwa ni mama yake lakini si sisi wanafunzi wala mwalimu.... Ndiyo ninayo, inabidi niipeleke kwa mwalimu lakini siwezi kuitoa barua hiyo hapa."
Nansisca(Rafiki wa karibu wa kike): "Mimi hata sijielewi, najiuliza kama nimlilie yeye au nijililie mwenyewe. Nilimpenda na naamini na yeye alinipenda pia lakini aliamua kunitesa. Hakutaka kunipa uhakika kwamba ananipenda.... Siwezi kumchukia lakini kama nisingejuana naye nina uhakika nisingefeli hivi.... Hapana, Rugame ndiye aliyekuwa akimkosesha raha na nadhani hata hili tukio, anaweza akawa amemsumbua sumbua sana kwa vile walishawahi kuahidiana hapo kabla kuhusu haya. "
Rugame(mwanafunzi mwenzake): "Inaniuma sana, siyo kwa sababu wenzangu wote wananitazama kwa jicho baya kwamba mimi ndiyo nimesababisha lakini inaniuma. Alikuwa ni mshindani wangu, katika kufanikiwa lazima kuwe na ushindani lakini kinachoniuma ni kwamba mwenzangu alimaanisha kile alichokisema. Mimi nilidhani ni kuwekeana chachu tu ya ushindani, kwamba hakuna ambaye angefanya aliyokuwa akisema... Ndiyo na inaniuma sana kwa sababu jana tu nilikutana naye na kumuambia ukweli kwamba ujinga wote tuliokuwa tumeongea mbele za watu na ahadi zote za kijinga kwamba tusifanye na alinielewa hata kwa mara ya kwanza tukakumbatiana lakini nashangaa leo amefanya hivi."
Mwanafunzi mwenzake: "Sikuwa karibu naye lakini najua wote darasani tulimpenda. Alikuwa kiongozi bora wa kuigwa... Kila alichokifanya kilikuwa na mafanikio. Wengi hatukuwa wa kufaulu hata kidogo lakini alituwezesha kupata japo 'D' moja. Kwa kweli nitamkumbuka sana."

Nilijiuliza mhusika ni nani huyo na kuanza kuifuatilia kiundani habari hiyo. Jina lake ni Kayumbas Mirambo na ameishi maisha waliyoishi watu wakubwa waliofanikiwa duniani na niliposikia habari zake, naona kwamba kila kitu kilichomfanya awe Kayumbas shujaa, mwanzo wake ni pale alipofaulu darasa la nne kwenda la tano. Ulikuwa mwanzo wa mikakati yake, mwanzo wa matumaini yake, mwanzo wa ushujaa wake na ndiyo mwanzo wa simulizi langu hili.

[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi