Wednesday, September 30, 2015

Damu Ya Ukoo Wangu: Sehemu ya 6



" Nashukuru tu Mungu mke wangu umenizalia kidume atakayeweza kuendeleza jina langu. Ni mtoto mzuri tu ambaye hatuna budi kumpokea kwa mikono minne, mi miwili na wewe miwili. Wewe umemuonaje?"
"Mimi nimemuona tofauti mume wangu."
Alisimama akisubiri nimuulize kwa nini jambo ambalo sikuligundua mapema na hivyo muda kupita kabla ya kumuuliza kwa nini na ndipo akanijibu,
"Samahani sana mume wangu nimekuzalia mtoto mlemavu. Inaniuma sana kushindwa kukuzalia mtoto kamilifu kama ulivyokuwa ukisubiria miaka yote tangu tulipooana."
"Mke wangu,.."
Niliita nikitaka kumkatisha kwani niliona si busara kumfanya ajione mwenye makosa mbele ya mipango ya Mungu. Tatizo langu lingejitokeza mbele nami nilikuwa nikiamini lenyewe haikuwa mipango ya Mungu bali ni shetani aliyelileta. Mke wangu baada ya kuona nataka kumkatisha, ndipo sauti yake ikaongezeka uchungu na kuendelea,
"Mume wangu najua jambo hilo limekuvunja sana moyo lakini tafadhali nipo chini ya miguu yako, naomba usimchukie mwanangu kwa kuwa ni kilema, mimi unaweza kunichukia lakini mwanangu hana makosa."
Hapo niligeuka na kulala kiubavu nikimtazama mke wangu kwa huruma. Nikaunyoosha mkono wangu kushika nywele zake nikizishika taratibu na kwa kujiamini nikamwambia,
"Siwezi kumchukia kwa vile ni kilema mke wangu, nakuhakikishia hilo. Wewe ondoa shaka kabisa kwenye jambo hilo."
"Ahsante mume wangu."
Sikusema kitu baada ya shukrani yake nami nikawa nikiwaza jinsi gani mke wangu alikuwa akijaribu kunifanya nimpende mtoto yule ambapo kiukweli nilishapoteza hamu ya kumpenda nikijua hakuwa mwanangu. Nililala tena chali na kuacha kumshika nywele. Baada ya kama dakika tano kupita bila ya kusemekana neno, mke wangu akaita,
"Mume wangu"
"Naam mke wangu"
Niliitika huku nikigeukia tena upande wake. Naye akaweka mkono wake shavuni kwangu na kuuliza,
"Mume wangu hivi kipi kilikukasirisha kule hospitali hadi ukaondoka?"
"Kwa nini unauliza mke wangu, sikukasirika kitu."
"Usinifiche mume wangu. Unajua namna ninavyokupenda mpenzi, nisingependa kukufanya ukasirike hata mara moja mume wangu. Niambie tu kama ni kwa sababu ya ukilema sema tu, mimi mbona ni muelewa."
"Aahsh"
Nilitoa pumzi kwanza kama vile mtu aliyeshangazwa na kuchoshwa sana na kisha nikamuambia,
"Mke wangu naomba uachane na hayo. Cha msingi ni kwamba sina hasira tena na haikuwa kwa vile mtoto ni kilema kwani kama ni ukilema basi bado ningekuwa na hasira maana ukilema haujatoka lakini ona ninavyofurahi mke wangu."
"Huniamini mume wangu. Hudhani kama naweza kukabiliana na kueleza ukweli ndiyo maana unanikwepa na kujaribu kupata ukweli kwa njia zingine."
"Ukweli upi?"
Nilishajua alichokuwa akiongelea ila kwa vile niliona ameanzisha mwenyewe, hivyo ni bora angemaliza mwenyewe.
"Najua unajiuliza kama kweli huyu mtoto ni wako au wa shemeji kwa vile amefanana zaidi na shemeji kuliko wewe."
"Si mimi tu, kila mtu atakayemuona atajiuliza hivyo hivyo kasoro nyie wawili tu."
"Shemeji hahusiki kabisa na mtoto huyu mume wangu, naomba uniamini. Nimekuwa mwaminifu kwako siku zote na hakuna mahusiano yoyote kati yangu na shemeji. Namuheshimu naye ananiheshimu sana. Huyu ni mtoto wetu mume wangu."
"Usijaribu kunishawishi mke wangu, kama ni kweli nitajua tu. Nisiijue damu yangu?"
"Haya usiku mwema lakini kumbuka huyu ni mwanao."
Nikiwa nimelala usiku wa manane, nilijigeuza mwili wangu nami nikahisi mkono wangu ukitua juu ya kitu fulani kigumu ambacho hakikuwa cha kawaida. Ubaridi nilioupata ulifanya macho yangu yafunguke ghafla na kuona vivuli viwili vya watu wakiwa wanamvuta mwanangu huku mke wangu akijitahidi kumzuia mtoto na kuniita kwa kelele. Kuitwa huko nilihisi tu kutokana na namna mke wangu alivyokuwa akitanua mdomo lakini haikutoka sauti yoyote. Watu hao tayari walishafika karibu na mlango wa chumbani naye mke wangu akiwa kama hatua mbili kutoka kitandani.
Niliamka kwa haraka lakini kabla sijafanikiwa kusimama, nikahisi mkono wangu ukivutwa kunizuia nisiende kumsaidia mke wangu. Niligeuka kwa hasira kuangalia nani aliyekuwa akinishika. Hapakuwa na mtu na si kwa sababu ya kuwa na giza bali kweli hapakuwa na mtu kwa maana hata kuona kivuli chake haikuwezekana.
Niliogopa sana na kujaribu kuuvuta mkono wangu kuhakikisha kama kweli nilikuwa nimevutwa na mtu asiyeonekana au ni mawazo yangu tu. Nilijaribu kuuvuta mkono wangu nami nikagundua kuwa kweli ulikuwa umeshikiliwa na mkono wa huyo mtu asiyeonekana, mikono iiyokomaa na ya baridi kama imewekwa kwenye jokofu. Mapigo ya moyo yalianza kwenda mbio kwani mke wangu alionekana kushindwa kuwazuia wale watu naye alikuwa akinitegemea mimi. Kwa namna alivyokuwa akiniangalia, alionesha kutokufurahishwa na kitendo cha mimi kutokwenda akishindwa kujua nilikuwa nimezuiliwa. Nilianza kuhisi moyo ukiniuma kwa hofu kuwa mke wangu angedhani nimefanya makusudi.
Ghafla nikasikia sauti ikininong'oneza,
"Usiende kumsaidia mkeo. Mnajitilia mikosi na huyo mtoto, siyo halali yenu huyo. Waachieni waende naye."

[Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]

Saturday, September 19, 2015

Jinsi ya kuipokea pole na kumfurahisha mtoaji pole...



Watu wengi katika taifa hili wamejiwekea mazoea hasi kwa jinsi yao ya kupokea pole. Wengine wamekwenda mbali zaidi kiasi cha kwamba kudhania kuwa wakiwa na matatizo, mtu wa karibu yao ni lazima atoe pole. Yaani wanachukulia kuambiwa pole ni haki yao na hivyo kukosa ustaarabu wa kuonesha kuheshimu huruma ya mtu atoaye pole.
Ukimuuliza mtu yoyote, ukiambiwa pole utajibu nini? Jibu lake bila shaka litakuwa ni ‘asante’. Jambo la kujiuliza ni kwamba, unaposema ‘asante’ baada ya kuambiwa pole, una uhakika ina utofauti na ile ya mtu akikuambia ‘hongera’? Katika hatua za kuboresha lugha yako ya kistaarabu, hasa kwa jinsi ya kuipokea pole, huo ndiyo mwanzo. Yaani hakikisha namna unavyoipokea pole kwa kusema ‘asante’ iwe tofauti na kama mtu angekuambia ‘hongera’ baada ya kufanikiwa jambo.
Katika kuimarika kwa lugha yako kwa jinsi ya kuipokea pole, basi ni vema uzingatie taratibu zile za kutoa pole katika nakala hizi. Yaani usitoe ‘asante’ tupu. Jambo unaloweza kuzingatia ili kufanikisha jitihada za kutotoa ‘asante’ tupu ni kugundua kuwa mpaka mtu anakuambia pole, basi ameguswa kwa namna fulani na matatizo yako. Asante yako ni vema ukailenga kwa namna mtu alivyoguswa na matatizo yako. Faida za kufanya hivi ni kumfanya mtu aliyetoa pole kuona kuwa umethamini mchango wake au hisia zake katika matatizo yako na kukufikiria kama mtu atayeweza kuthamini na kusaidia katika matatizo yake.
Katika hatua za mwanzo za kutotoa ‘asante’ tupu, unaweza kujifunza kutumia maneno, ‘asante au nashukuru kwa kuguswa.’ Hapo unamfanya mtu atoaye pole aamini kuwa hakufanya vile kana kwamba ni desturi bali moyo wake umekuwa wa kikarimu na kuweza kugundua au kuguswa na matatizo yako. Yaani si watu wote watakaotoa pole kwako, bali wachache kama yeye.
Zaidi ya kauli hiyo, ‘asante au nashukuru kwa kuguswa’, katika jinsi ya kuipokea pole unaweza kuivalisha ‘asante’ yako mavazi mazuri zaidi au ya kiufalme. Hapo ndipo unapoweza kupeleka mahusiano(urafiki) katika hatua nyingine au kufufua au kuimarisha uhusiano au urafiki. Hatua hii ya kuvalisha mavazi, si ya kuikimbilia kwa haraka kwani unapokosea, inaweza kuleta picha tofauti zaidi. Katika hatua za mwanzo, unaweza kutumia kauli zinazoendana na namna hii, ‘Nashukuru kwa kunifariji. Kiukweli unaelezea hali mbaya uliyokuwa nayo mwanzo na kisha kuelezea hali mpya iliyo bora baada ya kupokea pole’ au kauli ndogo kama ‘sikudhania kama jambo hili lingekugusa. Lakini nashukuru kwamba na wewe umeona jinsi gani linavyonisumbua…’
Nimalizie na kuvisha mavazi ya kiufalme ‘pole’ itokayo kwa mtu unayemjali sana, au mtu aliyetoa ‘pole’ ambayo maneno yake yalifanya usahau shida uliyo nayo, kwa jinsi hii ya kuipokea ‘pole’, ni vema kuitumia mara chache iwezekanavyo. Jinsi hii inakuwa na maelezo mengi ambayo yanazungumzia sifa za ujumla, labda baada ya mtu kuguswa mara nyingi na matatizo yako au kuonesha msaada mkubwa katika matatizo yako. Maelezo haya nahisi yashatumiwa mara nyingi na hivyo swala la kuyaainisha. Unaweza kusema kitu kinachoendana na ‘Nashukuru kwa kuguswa, tena nashukuru sana. Yaani katika watu wangu wa karibu, wewe…’
La kuzingatia: Hata uwe na matatizo kiasi gani, kupewa pole si haki yako. Hivyo ukipewa ‘pole’, shukuru. Ukiwa unapokea pole, jitahidi kujua nini kimemgusa mtu huyo hata kutoa pole na shukuru kufuatia kuguswa huko. Mfano katika msiba, mtu anaweza kuguswa kwa namna kifo kilivyotokea, au familia anayoiacha marehemu, au maisha aliyoishia marehemu(labda muda mfupi) n.k. lakini kwa namna yoyote ile, wataunganishwa na neon ‘pole’. Kazi yako ni kugundua kipi kimemgusa hasa. ‘Pole’ ya kipekee ni vema ikapokea shukrani ya kipekee, na ni vema kukumbuka ‘pole’ siyo ‘mchango wa kutatua matatizo’ ni kuguswa na kutoa kauli za kufariji.
Katika nakala ijayo katika mfululizo wa nakala hizi, jinsi ya kuomba radhi.

Sunday, September 13, 2015

Roho ya Kayumbas: Sehemu ya 7



Mwaka 2007

Siku ya kufunguliwa shule inapofika, Kayumbas na Jennifer wanaamka mnamo saa kumi na mbili kasorobo kama mwaka uliopita  na kwenda kuchota ndoo tatu za maji kila mmoja. Kisha wanajiandaa na shule na inapofika saa kumi na mbili na nusu wanamuamsha Mjanja ambaye tofauti na siku zingine ambazo alikuwa akichukua muda mrefu kuamka anapoamshwa, siku hiyo ananyanyuka kitandani baada ya kuitwa mara moja tu. Anamuamkia Kayumbas ambaye ndiye amemuamsha na kujiandaa haraka haraka akiwa na hamu isiyoelezeka ya kuanza shule.
Ifikapo saa moja kasorobo watoto wote wanakuwa tayari na wanamuaga mama yao kwenda shule. Mama Kayumbas anaishia kumuangalia mwanaye Mjanja anavyotembea huku akichomekea chomekea sare zake za shule za rangi ya bluu na begi lake dogo likiwa mgongoni. Mama Kayumbas anajichekea mwenyewe kwa kuona mwanaye akiwa na hamu hiyo kubwa ya kusoma na kutumaini kwamba atafika mbali kwenye masomo.
Kayumbas naye anafarijika kuanza mwaka huu kwani safari zake kati ya nyumbani na shule sasa hazitakuwa za umbali mrefu kama zamani kwa kuwa Majaliwa ameshahamia shule yao baada ya kuanza darasa la kwanza. Pia shule ya awali ya Mjanja haipo mbali na nyumbani kwao. Hivyo anauanza mwaka akiwa na matumaini zaidi hasa anapoona anakaribia kumaliza elimu yake ya msingi mwaka mmoja baadae.
Faraja hiyo ya Kayumbas inaendelea hata anapofika shule na kuungana na wanafunzi wengine kufanya usafi wa shule ikiwa ni kufagia madarasa na uwanja pamoja na kumwagia maji bustani za shule. Usafi unamalizika majira ya saa mbili asubuhi na kisha wanakwenda kwenye gwaride ambapo wanakaribishwa tena shule, wanatambulishwa walimu wapya wawili na kisha kuelekezwa madarasa watakayokuwa wakiyatumia.
Wanapotoka gwaride, wanafunzi wanaingia kwenye madarasa waliyoelekezwa na kuanza kugombaniana nafasi za kukaa na kuhamisha madawati kutoka madarasa yaliyokuwa na madawati ya ziada kwenda kwenye madarasa yenye upungufu wa madawati wakisimamiwa na walimu wao. Bado shule ina upungufu wa madawati na wanafunzi kulazimika kubanana hadi wanafunzi sita kwenye dawati la wanafunzi wanne.
Mpaka inapofika mida ya saa nne kamili wanafunzi wanakuwa wametulia kwenye madarasa yao na walimu wa madarasa ya la tano hadi la saba kuwapa wanafunzi wanaowaamini na wenye miandiko mizuri kuandika majina ya wanafunzi wote wa darasa husika kwenye daftari la mahudhurio. Wanafunzi wanajipanga kwenye mistari wakifuatisha mpangilio wa herufi za mwanzo za majina yao na kujiandikisha majina yao kwenye madaftari hayo, zoezi linalochukua kama nusu saa kumalizika.

"Mmh, Shoga! Huyu wewe au kopi yako?" Msichana mmoja kwenye dawati la mbele ya lile alilokaa Kayumbas anamuuliza mwenzake wakati akiiangalia picha ya rafiki yake huyo.
"Mimii huyoo. Yani siku hiyo ukumbini kila mtu alikuwa akitamani kunichombeza."
"Mmh, toka hukoo. Unapenda kujisifia sana shoga yangu. Yaani watu wasimuangalie..."
"Haa! Sasa unabisha?" Anatoa picha zingine na kumpa huku akimwambia,
"Haya hebu angalia mwenyewe picha hizo halafu uniambie kama kuna kasoro."
Wakati wale wasichana wakiendelea kusifiana, kwenye dawati alilokaa Kayumbas wenzake wawili wanakuwa wanaulizana,
"Halafu kamanda sijakuona kabisa likizo hii, siyo kawaida yako. Ulijichimbia wapi kamanda?"
"Aaah, Tanga hiyo mzee."
"Duuh, na wewe mshikaji umefikia kwenda Tanga? Kweli dunia imeisha. Nani huyo ulienda kumpiga ndumba?(kumroga)"
"Ndumba wapii? Mabinti wa Kitangaa, ooh, wanajua kujipamba, ooh, kwa mapozi wanatambaa, kwa mapenzi mi nitawafuata Tangaa"
"Mmh, wimbo nishausahau huo wewe bado unaukumbuka tu?"
Kabla ya kumjibu mwenzake anakatishwa na Kayumbas anayemstua na kumuuliza,
"Oya, twisheni ilikuwaje likizo?"
"Thafi tu mshikaji."
"Oya nilishakuambia utani huo thipendi."
"Utani ufanyaje?"
Yule mwenzao wa pembeni naye anaingilia kwa kumuonya mwenzake,
"Kamanda acha kumzingua Kayumbas bwana."
"Hamna uthinimaindi wala nini Kayumbas, mimi nakutania tu kwa kuwa wewe mshikaji wangu yani. Yani nakufili ile kinyama, wewe hujui tu."
"Poa yaishe, niazime madaftari yako ya twisheni."
"Sasa hapa thina mshikaji, nitakuletea kesho."
"Wewe endelea tu, thiku utashangaa nakuthemea kwa mwalimu."
Kayumbas anaachana nao na wao kuendelea kupigiana hadithi za Tanga na za yaliyotokea kipindi cha twisheni na zamu ya kufanya usafi shuleni.
Dakika kumi na tatu kabla ya kufika saa saba kamili ambao ndio muda wa masomo kuisha, anaingia mwalimu mmoja ambaye ni maarufu miongoni mwa wanafunzi hata kwa wale ambao hajawahi kuwafundisha. Ni mwalimu mwenye urefu wa wastani, mnene kidogo na umri kati ya miaka thelathini hadi arobaini. Kinachompa umaarufu shuleni ni vitu viwili, ukali na mavazi yake japokuwa tabia yake ya kuvaa sketi fupi ndiyo hasa iliyowafanya wanafunzi kutaka kumjua pale tu wamuonapo mara ya kwanza.
"Moja... mbili... tatu." Anasema kiranja wa darasa mara mwalimu huyo anapoingia darasani na wanafunzi wote wanasimama na kusema kwa pamoja,
"Elimuu ni msingii wa maiisha. Shikaamoo mwaaalim."
"Marahaba, hamjambo?"
"Hatujamboo mwaalim."
Mwalimu huyo anapita mpaka mbele ya darasa na kuandika tarehe ya siku hiyo ubaoni na kuchora mstari wa pambizo kabla ya kuwageukia wanafunzi na kuwaambia,
"Haya kaeni chini. Mimi ndiye nitakayekuwa nikiwafundisha somo la Maarifa ya Jamii na huwa sipendelei kusumbuana na wanafunzi. Si mmeshasikia habari zangu kutoka kwa kaka na dada zenu?"
"Ndiyoo."
Mara minong'ono inaanza kwa baadhi ya wanafunzi wakiwaelezea wenzao yale waliyoyasikia kuhusu mwalimu huyo na bila ya kupoteza hata sekunde mwalimu anaikemea,
"Nadhani hamjanijua nyie. Nikiwa darasani sitaki kusikia minong'ono ya aina yoyote ile. Siyo kuongea, mnielewe vizuri hapo, hata ile minong'ono siitaki. Nina aleji na kelele."
"Hahaha" Baadhi ya wanafunzi wanacheka na mwalimu anaendelea,
"Haya, nimeuliza kama mmesikia kuhusu mimi mkasema ndiyo, sasa kama hulijui jina langu wewe mwenyewe simama juu."
Wanasimama wanafunzi wanaokaribia ishirini kati ya wanafunzi wote tisini na mbili wa darasa hilo ukiwa ndiyo mkondo wenye wanafunzi wachache kuliko mikondo yote minne ya darasa la sita. Anawatazama wanafunzi hao kama vile akiwashangaa na kumwambia mwanafunzi mmoja aliyekuwa amesimama kutoka dawati la mbele,
"Hebu nenda pale ofisi ya walimu uulizie meza ya Madam" Anavuta sekunde kadhaa bila ya kusema neno na kuwageukia wanafunzi wengine waliokaa na kuwauliza, "Madam nani kwa nyie mnaonijua?"
"Madam Pendeeekiiii." Wanafunzi wachache wanajibu kwa sauti ya juu, wakijivunia kumjua mwalimu huyo kwa wale wasiomjua.
"Umesikia? Ulizia meza ya Madam Pendeki, kuna mwanzi wangu juu ya meza uniletee nipate wa kuwasimulia wenzao. Si huwa mnalinganisha fimbo za walimu kujua zipi zinauma sana, na mimi nataka mnilinganishe sasa."
Wanafunzi waliosimama kwa waliokaa wanaanza kutahamaki na kumuogopa mwalimu huyo.

[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]
  • Hadithi na Simulizi