Monday, September 7, 2015

Jinsi ya kusimulia vichekesho kwa namna itakayochekesha…



Katika nakala iliyopita katika mfululizo wa nakala hizi, nilizungumzia umuhimu wa kujua kuchekesha bila ya kukariri vichekesho. Lakini, inanipasa kuelezea namna ya kutumia vichekesho katika kuchekesha kwani ndiyo mwanzo wa kujijengea uwezo wa kuchekesha bila kufikiria. Kabla sijaanza kuelezea namna ya kutumia vichekesho ili kuchekesha, nikumbushe kuwa vichekesho kama mpangilio wa maneno pekee, vina mchango mdogo sana katika kuchekesha.
Kama umewahi kuona watu wakielezea jambo na kujikuta wakicheka wenyewe bila ya kukufanya wewe ucheke, jua watu hao walishindwa kuvitumia vichekesho hivyo kuchekesha. Pia, wapo wanaokujulisha kuwa wanatoa vichekesho ili kuchekesha lakini hata wanapomaliza kuelezea vichekesho hivyo, msikilizaji unashindwa kuona kitu cha kuchekesha. Sina shaka kwamba kila mtu ameshatokewa na hilo. Baadhi hujaribu kuelezea zaidi vichekesho vyao pale wanapomaliza na kushindwa kuchekesha lakini hata kwa maelezo ya mara ya pili, bado wapo ambao hufeli kutumia vichekesho hivyo kuchekesha.
Kitu cha kwanza kabisa cha kuzingatia, ni kujua nini hasa ndiyo chanzo cha maelezo fulani kuwa vichekesho. Lazima ujue nini kilichokufanya wewe uelewe kuwa maelezo fulani ni vichekesho na mengine si vichekesho. Pia kama nilivyoelezea katika nakala zilizopita katika mfululizo huu, lazima ujue ni hatua ipi kati ya zile hatua kuu tatu za kufanya mtu acheke ndipo vichekesho hivyo utakavyotumia vitamhakikishia mtu kuwa ni vichekesho.
Chanzo cha kuchekesha kwa vichekesho, mara nyingi huwa ni mhusika ndani ya kichekesho kuelewa tofauti jambo fulani mfano katika kichekesho kimoja, mteja wa kiume kufurahia kusikia atapewa kampani na sekretari wakati bosi akifanya shughuli nyingine lakini sekretari kumbe ni wa kiume na si wa kike au kichekesho kingine ni mchina kupewa jukumu la ‘supplies’ yaani mahitaji na badala yake yeye kuelewa kuwa jukumu lake ni kufanya ‘surprise’ yaani jambo zuri lisilotarajiwa..
Pia katika kutambua hatua gani hasa ndiyo mihimili ya vichekesho, mara nyingi huwa ni katika ule muda ambao mchekeshwaji anahusisha matokeo ya vichekesho yaani mwisho wa vichekesho na ile picha au mwisho ambao yeye aliutabiri, ni vema kuhakikisha kuwa usimuliaji wako wa vichekesho, hauingilii hatua hiyo kwa kujaribu kuchekesha kabla ya hiyo hatua.
Kwa kutambua chanzo, ni lazima umuwezeshe mlengwa kubaini chanzo kama ulivyoona wewe msimuliaji. Yaani kwa mifano ya hapo juu, lazima uhakikishe mlengwa anatambua kuwa kuna ‘supplies’ na ‘surprise’ zenye matamshi yanayoendana lakini maana tofauti na kama kuna sekretari wa kike na wa kiume kabla ya kufika kwa hatua uliyobaini kuwa ndipo kuchekesha kutatokea.
Wanachokosea wengi ni kudhani mlengwa ana uelewa kama aliokuwa nao yeye anayetoa vichekesho. Pia mazingira yanapokuwa tofauti, labda vichekesho wewe ulivisoma lakini sasa unasimulia, au wewe ulihusika katika vichekesho lakini sasa unamuelezea mtu ambaye atakuwa msikilizaji tu, na namna nyingine nyingi. Hivyo jambo kuu au mzizi wa yote ni kujiuliza mara mbili mbili, je mazingira na uelewa uliokuwa nao wakati ukivipata vichekesho hivyo, ndiyo mazingira na uelewa uliopo wakati unavitoa vichekesho hivyo? Mambo hayo yanapoendana, nina imani kuwa vichekesho vyako vitafanya kazi yake ya kuchekesha.
Katika nakala inayofuata katika mfululizo wa nakala hizi tutaangalia mambo ya kuepuka wakati wa kutoa vichekesho… mifano iliyoelezewa hapo juu imetolewa kwa kirefu katika facebook group, www.facebook.com/copykennytz

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi