" Nashukuru tu
Mungu mke wangu umenizalia kidume atakayeweza kuendeleza jina langu. Ni mtoto
mzuri tu ambaye hatuna budi kumpokea kwa mikono minne, mi miwili na wewe
miwili. Wewe umemuonaje?"
"Mimi nimemuona
tofauti mume wangu."
Alisimama akisubiri
nimuulize kwa nini jambo ambalo sikuligundua mapema na hivyo muda kupita kabla
ya kumuuliza kwa nini na ndipo akanijibu,
"Samahani sana
mume wangu nimekuzalia mtoto mlemavu. Inaniuma sana kushindwa kukuzalia mtoto
kamilifu kama ulivyokuwa ukisubiria miaka yote tangu tulipooana."
"Mke
wangu,.."
Niliita nikitaka
kumkatisha kwani niliona si busara kumfanya ajione mwenye makosa mbele ya
mipango ya Mungu. Tatizo langu lingejitokeza mbele nami nilikuwa nikiamini
lenyewe haikuwa mipango ya Mungu bali ni shetani aliyelileta. Mke wangu baada
ya kuona nataka kumkatisha, ndipo sauti yake ikaongezeka uchungu na kuendelea,
"Mume wangu najua
jambo hilo limekuvunja sana moyo lakini tafadhali nipo chini ya miguu yako,
naomba usimchukie mwanangu kwa kuwa ni kilema, mimi unaweza kunichukia lakini
mwanangu hana makosa."
Hapo niligeuka na
kulala kiubavu nikimtazama mke wangu kwa huruma. Nikaunyoosha mkono wangu
kushika nywele zake nikizishika taratibu na kwa kujiamini nikamwambia,
"Siwezi kumchukia
kwa vile ni kilema mke wangu, nakuhakikishia hilo. Wewe ondoa shaka kabisa
kwenye jambo hilo."
"Ahsante mume
wangu."
Sikusema kitu baada ya
shukrani yake nami nikawa nikiwaza jinsi gani mke wangu alikuwa akijaribu
kunifanya nimpende mtoto yule ambapo kiukweli nilishapoteza hamu ya kumpenda
nikijua hakuwa mwanangu. Nililala tena chali na kuacha kumshika nywele. Baada
ya kama dakika tano kupita bila ya kusemekana neno, mke wangu akaita,
"Mume wangu"
"Naam mke
wangu"
Niliitika huku
nikigeukia tena upande wake. Naye akaweka mkono wake shavuni kwangu na kuuliza,
"Mume wangu hivi
kipi kilikukasirisha kule hospitali hadi ukaondoka?"
"Kwa nini unauliza
mke wangu, sikukasirika kitu."
"Usinifiche mume
wangu. Unajua namna ninavyokupenda mpenzi, nisingependa kukufanya ukasirike
hata mara moja mume wangu. Niambie tu kama ni kwa sababu ya ukilema sema tu,
mimi mbona ni muelewa."
"Aahsh"
Nilitoa pumzi kwanza
kama vile mtu aliyeshangazwa na kuchoshwa sana na kisha nikamuambia,
"Mke wangu naomba
uachane na hayo. Cha msingi ni kwamba sina hasira tena na haikuwa kwa vile
mtoto ni kilema kwani kama ni ukilema basi bado ningekuwa na hasira maana
ukilema haujatoka lakini ona ninavyofurahi mke wangu."
"Huniamini mume
wangu. Hudhani kama naweza kukabiliana na kueleza ukweli ndiyo maana unanikwepa
na kujaribu kupata ukweli kwa njia zingine."
"Ukweli upi?"
Nilishajua alichokuwa
akiongelea ila kwa vile niliona ameanzisha mwenyewe, hivyo ni bora angemaliza
mwenyewe.
"Najua unajiuliza
kama kweli huyu mtoto ni wako au wa shemeji kwa vile amefanana zaidi na shemeji
kuliko wewe."
"Si mimi tu, kila
mtu atakayemuona atajiuliza hivyo hivyo kasoro nyie wawili tu."
"Shemeji hahusiki
kabisa na mtoto huyu mume wangu, naomba uniamini. Nimekuwa mwaminifu kwako siku
zote na hakuna mahusiano yoyote kati yangu na shemeji. Namuheshimu naye
ananiheshimu sana. Huyu ni mtoto wetu mume wangu."
"Usijaribu
kunishawishi mke wangu, kama ni kweli nitajua tu. Nisiijue damu yangu?"
"Haya usiku mwema
lakini kumbuka huyu ni mwanao."
Nikiwa nimelala usiku
wa manane, nilijigeuza mwili wangu nami nikahisi mkono wangu ukitua juu ya kitu
fulani kigumu ambacho hakikuwa cha kawaida. Ubaridi nilioupata ulifanya macho
yangu yafunguke ghafla na kuona vivuli viwili vya watu wakiwa wanamvuta
mwanangu huku mke wangu akijitahidi kumzuia mtoto na kuniita kwa kelele. Kuitwa
huko nilihisi tu kutokana na namna mke wangu alivyokuwa akitanua mdomo lakini
haikutoka sauti yoyote. Watu hao tayari walishafika karibu na mlango wa
chumbani naye mke wangu akiwa kama hatua mbili kutoka kitandani.
Niliamka kwa haraka
lakini kabla sijafanikiwa kusimama, nikahisi mkono wangu ukivutwa kunizuia
nisiende kumsaidia mke wangu. Niligeuka kwa hasira kuangalia nani aliyekuwa
akinishika. Hapakuwa na mtu na si kwa sababu ya kuwa na giza bali kweli
hapakuwa na mtu kwa maana hata kuona kivuli chake haikuwezekana.
Niliogopa sana na
kujaribu kuuvuta mkono wangu kuhakikisha kama kweli nilikuwa nimevutwa na mtu
asiyeonekana au ni mawazo yangu tu. Nilijaribu kuuvuta mkono wangu nami
nikagundua kuwa kweli ulikuwa umeshikiliwa na mkono wa huyo mtu asiyeonekana,
mikono iiyokomaa na ya baridi kama imewekwa kwenye jokofu. Mapigo ya moyo
yalianza kwenda mbio kwani mke wangu alionekana kushindwa kuwazuia wale watu
naye alikuwa akinitegemea mimi. Kwa namna alivyokuwa akiniangalia, alionesha
kutokufurahishwa na kitendo cha mimi kutokwenda akishindwa kujua nilikuwa
nimezuiliwa. Nilianza kuhisi moyo ukiniuma kwa hofu kuwa mke wangu angedhani
nimefanya makusudi.
Ghafla nikasikia sauti
ikininong'oneza,
"Usiende kumsaidia
mkeo. Mnajitilia mikosi na huyo mtoto, siyo halali yenu huyo. Waachieni waende
naye."
[Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia
simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]
No comments:
Post a Comment