Mwaka
2007
Siku ya kufunguliwa
shule inapofika, Kayumbas na Jennifer wanaamka mnamo saa kumi na mbili kasorobo
kama mwaka uliopita na kwenda kuchota
ndoo tatu za maji kila mmoja. Kisha wanajiandaa na shule na inapofika saa kumi
na mbili na nusu wanamuamsha Mjanja ambaye tofauti na siku zingine ambazo alikuwa
akichukua muda mrefu kuamka anapoamshwa, siku hiyo ananyanyuka kitandani baada
ya kuitwa mara moja tu. Anamuamkia Kayumbas ambaye ndiye amemuamsha na
kujiandaa haraka haraka akiwa na hamu isiyoelezeka ya kuanza shule.
Ifikapo saa moja
kasorobo watoto wote wanakuwa tayari na wanamuaga mama yao kwenda shule. Mama Kayumbas
anaishia kumuangalia mwanaye Mjanja anavyotembea huku akichomekea chomekea sare
zake za shule za rangi ya bluu na begi lake dogo likiwa mgongoni. Mama Kayumbas
anajichekea mwenyewe kwa kuona mwanaye akiwa na hamu hiyo kubwa ya kusoma na
kutumaini kwamba atafika mbali kwenye masomo.
Kayumbas naye
anafarijika kuanza mwaka huu kwani safari zake kati ya nyumbani na shule sasa
hazitakuwa za umbali mrefu kama zamani kwa kuwa Majaliwa ameshahamia shule yao
baada ya kuanza darasa la kwanza. Pia shule ya awali ya Mjanja haipo mbali na
nyumbani kwao. Hivyo anauanza mwaka akiwa na matumaini zaidi hasa anapoona
anakaribia kumaliza elimu yake ya msingi mwaka mmoja baadae.
Faraja hiyo ya Kayumbas
inaendelea hata anapofika shule na kuungana na wanafunzi wengine kufanya usafi
wa shule ikiwa ni kufagia madarasa na uwanja pamoja na kumwagia maji bustani za
shule. Usafi unamalizika majira ya saa mbili asubuhi na kisha wanakwenda kwenye
gwaride ambapo wanakaribishwa tena shule, wanatambulishwa walimu wapya wawili
na kisha kuelekezwa madarasa watakayokuwa wakiyatumia.
Wanapotoka gwaride,
wanafunzi wanaingia kwenye madarasa waliyoelekezwa na kuanza kugombaniana
nafasi za kukaa na kuhamisha madawati kutoka madarasa yaliyokuwa na madawati ya
ziada kwenda kwenye madarasa yenye upungufu wa madawati wakisimamiwa na walimu
wao. Bado shule ina upungufu wa madawati na wanafunzi kulazimika kubanana hadi
wanafunzi sita kwenye dawati la wanafunzi wanne.
Mpaka inapofika mida ya
saa nne kamili wanafunzi wanakuwa wametulia kwenye madarasa yao na walimu wa
madarasa ya la tano hadi la saba kuwapa wanafunzi wanaowaamini na wenye
miandiko mizuri kuandika majina ya wanafunzi wote wa darasa husika kwenye
daftari la mahudhurio. Wanafunzi wanajipanga kwenye mistari wakifuatisha
mpangilio wa herufi za mwanzo za majina yao na kujiandikisha majina yao kwenye
madaftari hayo, zoezi linalochukua kama nusu saa kumalizika.
"Mmh, Shoga! Huyu
wewe au kopi yako?" Msichana mmoja kwenye dawati la mbele ya lile alilokaa
Kayumbas anamuuliza mwenzake wakati akiiangalia picha ya rafiki yake huyo.
"Mimii huyoo. Yani
siku hiyo ukumbini kila mtu alikuwa akitamani kunichombeza."
"Mmh, toka hukoo.
Unapenda kujisifia sana shoga yangu. Yaani watu wasimuangalie..."
"Haa! Sasa
unabisha?" Anatoa picha zingine na kumpa huku akimwambia,
"Haya hebu angalia
mwenyewe picha hizo halafu uniambie kama kuna kasoro."
Wakati wale wasichana
wakiendelea kusifiana, kwenye dawati alilokaa Kayumbas wenzake wawili wanakuwa
wanaulizana,
"Halafu kamanda
sijakuona kabisa likizo hii, siyo kawaida yako. Ulijichimbia wapi kamanda?"
"Aaah, Tanga hiyo
mzee."
"Duuh, na wewe
mshikaji umefikia kwenda Tanga? Kweli dunia imeisha. Nani huyo ulienda kumpiga
ndumba?(kumroga)"
"Ndumba wapii?
Mabinti wa Kitangaa, ooh, wanajua kujipamba, ooh, kwa mapozi wanatambaa, kwa
mapenzi mi nitawafuata Tangaa"
"Mmh, wimbo
nishausahau huo wewe bado unaukumbuka tu?"
Kabla ya kumjibu
mwenzake anakatishwa na Kayumbas anayemstua na kumuuliza,
"Oya, twisheni
ilikuwaje likizo?"
"Thafi tu
mshikaji."
"Oya
nilishakuambia utani huo thipendi."
"Utani ufanyaje?"
Yule mwenzao wa pembeni
naye anaingilia kwa kumuonya mwenzake,
"Kamanda acha
kumzingua Kayumbas bwana."
"Hamna
uthinimaindi wala nini Kayumbas, mimi nakutania tu kwa kuwa wewe mshikaji wangu
yani. Yani nakufili ile kinyama, wewe hujui tu."
"Poa yaishe,
niazime madaftari yako ya twisheni."
"Sasa hapa thina
mshikaji, nitakuletea kesho."
"Wewe endelea tu,
thiku utashangaa nakuthemea kwa mwalimu."
Kayumbas anaachana nao
na wao kuendelea kupigiana hadithi za Tanga na za yaliyotokea kipindi cha
twisheni na zamu ya kufanya usafi shuleni.
Dakika kumi na tatu
kabla ya kufika saa saba kamili ambao ndio muda wa masomo kuisha, anaingia
mwalimu mmoja ambaye ni maarufu miongoni mwa wanafunzi hata kwa wale ambao hajawahi
kuwafundisha. Ni mwalimu mwenye urefu wa wastani, mnene kidogo na umri kati ya
miaka thelathini hadi arobaini. Kinachompa umaarufu shuleni ni vitu viwili,
ukali na mavazi yake japokuwa tabia yake ya kuvaa sketi fupi ndiyo hasa
iliyowafanya wanafunzi kutaka kumjua pale tu wamuonapo mara ya kwanza.
"Moja... mbili...
tatu." Anasema kiranja wa darasa mara mwalimu huyo anapoingia darasani na
wanafunzi wote wanasimama na kusema kwa pamoja,
"Elimuu ni msingii
wa maiisha. Shikaamoo mwaaalim."
"Marahaba,
hamjambo?"
"Hatujamboo
mwaalim."
Mwalimu huyo anapita
mpaka mbele ya darasa na kuandika tarehe ya siku hiyo ubaoni na kuchora mstari
wa pambizo kabla ya kuwageukia wanafunzi na kuwaambia,
"Haya kaeni chini.
Mimi ndiye nitakayekuwa nikiwafundisha somo la Maarifa ya Jamii na huwa
sipendelei kusumbuana na wanafunzi. Si mmeshasikia habari zangu kutoka kwa kaka
na dada zenu?"
"Ndiyoo."
Mara minong'ono inaanza
kwa baadhi ya wanafunzi wakiwaelezea wenzao yale waliyoyasikia kuhusu mwalimu
huyo na bila ya kupoteza hata sekunde mwalimu anaikemea,
"Nadhani
hamjanijua nyie. Nikiwa darasani sitaki kusikia minong'ono ya aina yoyote ile.
Siyo kuongea, mnielewe vizuri hapo, hata ile minong'ono siitaki. Nina aleji na
kelele."
"Hahaha"
Baadhi ya wanafunzi wanacheka na mwalimu anaendelea,
"Haya, nimeuliza
kama mmesikia kuhusu mimi mkasema ndiyo, sasa kama hulijui jina langu wewe
mwenyewe simama juu."
Wanasimama wanafunzi
wanaokaribia ishirini kati ya wanafunzi wote tisini na mbili wa darasa hilo
ukiwa ndiyo mkondo wenye wanafunzi wachache kuliko mikondo yote minne ya darasa
la sita. Anawatazama wanafunzi hao kama vile akiwashangaa na kumwambia
mwanafunzi mmoja aliyekuwa amesimama kutoka dawati la mbele,
"Hebu nenda pale
ofisi ya walimu uulizie meza ya Madam" Anavuta sekunde kadhaa bila ya
kusema neno na kuwageukia wanafunzi wengine waliokaa na kuwauliza, "Madam
nani kwa nyie mnaonijua?"
"Madam Pendeeekiiii."
Wanafunzi wachache wanajibu kwa sauti ya juu, wakijivunia kumjua mwalimu huyo
kwa wale wasiomjua.
"Umesikia? Ulizia
meza ya Madam Pendeki, kuna mwanzi wangu juu ya meza uniletee nipate wa
kuwasimulia wenzao. Si huwa mnalinganisha fimbo za walimu kujua zipi zinauma
sana, na mimi nataka mnilinganishe sasa."
Wanafunzi waliosimama
kwa waliokaa wanaanza kutahamaki na kumuogopa mwalimu huyo.[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]
No comments:
Post a Comment