Saturday, September 5, 2015

Damu ya Ukoo Wangu: Sehemu ya 5

Bia pamoja na mziki wa taratibu uliokuwa ukipigwa kwenye baa hiyo vilinisaidia kupoteza muda na mawazo lakini kabla ya kufikia hali ya kutokujitambua, nilipata wazo la kwenda kuwafukuza wote wawili pale nyumbani. Niliondoka kwenye baa hiyo nikijiongelea na kujisikitikia mwenyewe hadi nilipofika nyumbani. Niliwakuta Shukuru na Lilian wakiwa wameshawasili pamoja na yule mdogo wake mke wangu, Jeni. Pia palikuwa na ndugu zake wengine  mke wangu pamoja na baadhi ya majirani na kufanya sebule ionekane haitoshi. Idadi kubwa ya wageni pale nyumbani ilinifanya niigize kana kwamba hakukuwa na tatizo kwani niliamini hakukuwa na mtu mwingine aliyegundua kwa sababu walimuona mtoto kwa mbali tu tena wale wachache waliolazimisha kumchungulia chumbani alikolazwa yule mtoto.
Nilipokea hongera zote nilizokuwa nikipewa na wageni nami pamoja na mke wangu tulikuwa tukiungana nao kumshukuru Mungu kwa kutujalia kupata mtoto lakini moyoni mwangu nilikuwa nikitafuta muda wa kuweza kuyamaliza matatizo yangu. Wakati wageni wakiendelea kufika mmoja mmoja, mdogo wangu aliniita kwa upole tuweze kutoka nje. Nikijua alichotaka kunieleza  na kwa vile nilikuwa nikiutaka mwanya huo, nilimfuata kwa haraka nasi tukaenda mpaka chumbani kwake.
"Kaka, inabidi tu kumshukuru Mungu kwa yote anayokujalia. Kwanza mkeo kushika mimba muda wote hata akajifungua salama ni jambo la kushukuru sana maana si wote wanaofanikiwa kufikia hapo. Najua kibinadamu hakuna aliyetegemea ulemavu lakini yote hiyo ni mipango ya Mungu, hakunala kufanya zaidi tu ya kumshukuru yeye."
Sikuamini kama wazo kubwa la mdogo wangu halikuwa kwenye kufanana sura na mwanangu bali ulemavu wake. Baada ya kumaliza kauli yake, sikuwa na hamu ya kujibu chochote nami niliishia tu kumtazama usoni nikishindwa kummaliza hadi aliponiuliza,
"Vipi kwani kaka, mbona hivyo?"
"Umemuona sura yule mtoto?"
Kwa mshangao mkubwa, akanijibu
"Ndiyo, kwani ina kasoro? Afu amekuchukua sura yako kabisa akaiacha ya mama yake."
Ilipita kama dakika moja nikiitafakari kauli yake kichwani huku sehemu zingine za mwili zikikusanya nguvu na baada ya kukusanya nguvu za kutosha, nilijikuta nikisimama na kumvamia mdogo wangu huku nikimkunja shingoni na kwa hasira nikafoka,
"Umewezaje kunisaliti Shukuru? Yani umesema unakaa kwa shughuli zako kumbe nia yako ni kutembea na mke wangu? Umewe..."
"Kaka, mimi nimetembea na mke wako?"
"Unaniuliza mimi! Mtoto amewaumbua huyu."
"Mungu wangu, yaani Baraka umefikia kunifikiria hivyo mimi? Mimi siwezi ..."
Ilimbidi asimame maana kulikuwa na hodi mlangoni kwake na alipofungua ndugu mmoja wa mke wangu alitutaarifu kuwa chai ilikuwa ipo tayari. Baada tu ya kuurudishia mlango, Shukuru akaniambia,
"Siwezi nikatembea na mke wako Baraka. Kama unaona sura inafanana zaidi na mimi ni upofu wako tu maana hata mimi na wewe tunafanana."
Sikutaka kuendeleza mazungumzo yaliyokuwa hayana dalili za kufikia mwisho na kwa vile nilitaka niende kazini, nikaenda hadi mlangoni alipokuwa amesimama na huku nikitazamana naye usoni nikamwambia,
"Ukweli nitaujua tu Shukuru na niamini mimi, utajuta milele ikiwa kweli."
Nilipoingia ndani ya nyumba yetu nilikwenda kwenye chumba cha kulia chakula na kupata kifungua kinywa. Kwa vile mke wangu alikuwa akiongea na wageni, sikutaka kumtoa kwenye mazungumzo lakini nilipoingia chumbani kujiandaa kwenda kazini, mke wangu naye aliingia na swali lake la kwanza likawa,
"Mbona hivyo mume wangu? Tumekwenda wote hospitali lakini kurudi ukatukimbia. Kweli yani shemeji yeye ndiyo wa kunirudisha..."
Alishindwa kuendelea baada ya uchungu kumjaa na kumfanya atoe chozi. Huruma iliniingia ghafla na hasa sikutaka wageni wahisi kama kuna kitu hakipo sawa. Hivyo nikakaa pembeni yake kitandani na kumkumbatia nikimwambia,
"Samahani mke wangu, sikupenda kufanya hivyo na nashindwa kuelewa kwa nini niliwahi kuondoka hospitali. Tafadhali naomba usinifikirie vibaya kabisa. Nakupenda sana mke wangu na sasa tumeanzisha familia yenye watoto, naomba tuwe watu wa furaha kwa yote yale Mungu anayotujalia."
Mke wangu aliniangalia shingo upande huku akitia huruma. Nikiwa na hofu kama ameweza kugundua uwongo ndani yangu, nikaamua kumuaga,
"Mke wangu, acha mimi niende kazini sasa. Hongera kwa kujifungua salama, naomba uniangalizie mtoto wangu."
Kabla ya kuanza kuondoka nikambusu kwenye paji la uso na ndipo taratibu nikauelekea mlango huku moyoni nikijalaumu kwa uwongo wote niliousema kwake na kisha kwenda kazini.
Siku iliendelea kwa namna hiyo, kazini nikipokea hongera nyingi kutoka kwa wenzangu na simu nyingi za pongezi kutoka kwa watu mbalimbali ambapo kila pongezi niliyokuwa nikiipokea, moyoni nilikuwa nikijiuliza watu hao wangesemaje endapo wangeelewa yaliyotokea. Maswali hayo yalinitia hasira kwani niliamini watu hao wangeniona mimi mjinga na si kunionea huruma endapo wangeujua ukweli.
Usiku ulipofika nikiwa chumbani na mke wangu tayari kwa kulala, ndipo mke wangu akaanzisha tena mazungumzo juu ya yule mtoto.
"Mume wangu, hatukupata muda wa kuzungumza kuhusu mtoto wetu. Niambie umemuonaje?"
Nilitamani niuone uso wa mke wangu vizuri jinsi anavyoongea lakini kwa vile taa zilikuwa zimezimwa, giza likaninyima uwezo huo. Nikiwa bado njia panda kama huo ndiyo ulikuwa muda muafaka wa kumuelezea mke wangu wasiwasi wangu au la, nikatoa jibu lisilofungamana na upande wowote.
" Nashukuru tu Mungu mke wangu umenizalia kidume atakayeweza kuendeleza jina langu. Ni mtoto mzuri tu ambaye hatuna budi kumpokea kwa mikono minne, mi miwili na wewe miwili. Wewe umemuonaje?"
"Mimi nimemuona tofauti mume wangu.”

[Nini kitafuata..? Endelea kufuatilia simulizi hili. Pia nakala zipo tayari madukani.]

No comments:

Post a Comment

  • Hadithi na Simulizi