Saturday, September 5, 2015

Roho ya Kayumbas: Sehemu ya 5

Muda wa kurudi nyumbani pia unapofika, Kayumbas inabidi ashuke vituo viwili kabla ya kufika kituo cha nyumbani kwao kwa ajili ya kumpitia Majaliwa na ndipo arudi naye nyumbani.
Wanapofika nyumbani siku hiyo, mama yake anamsimamisha Kayumbas asile kwanza akamtafute mdogo wake wa mwisho, Mjanja kwani tangu saa nne asubuhi ya siku hiyo hakuonekana nyumbani.
Kayumbas anabadili nguo zake kwa haraka na kwenda kwa majirani kuanza kumuulizia mdogo wake. Anazunguka kwenye nyumba mbili tatu alizozipa nafasi kubwa ya mdogo wake kuwepo humo na kwenye nyumba ya tatu anamkuta akiwa amekaa na baadhi ya watoto wengine wakiangalia filamu ya ngumi iliyotafasiriwa kwa kiswahili.
Kayumbas anamuita mdogo wake huyo na kwenda naye moja kwa moja nyumbani bila ya kumlaumu chochote lakini anapofika nyumbani, anakaribishwa na swali la tahamaki kubwa kutoka kwa mama yake.
"Wee! Umemkuta wapi?"
"Alikuwa kwa akina Kuruthumu." Kayumbas anahisi mikono ya mdogo wake ikianza kutetemeka na kuiachia kabla ya mama yake kumuuliza swali lingine.
"Alikuwa anaangalia video, si ndiyo?"
"Nilimkuta anacheza na wenzake thebuleni." Kayumbas anajaribu kumtetea mdogo wake.
"Wewe, ulikuwa unaangalia video eh?" Mama Kayumbas anamfuata Mjanja huku akiwa ameshika fimbo mkononi na kumuuliza kwa ukali.
"Mmm mmm mm." Mjanja anatingisha kichwa kukataa huku machozi yakimlengalenga.
"Wewe ulikuwa unaangalia picha la Van Dame si ndiyo?"
"Aa aa, sijaangalia kitu mimi unanionea." Anajaribu kukataa na mama yake anamuuliza tena,
"Niambie umeangalia picha gani?"
"Siijui."
"Manachulye litondo." Anasema mama Kayumbas kwa hasira na akipunguza ukali wa sauti yake anasema, "Nilijua tu, na wewe Kayumbas unajaribu kunidanganya. Utampoteza mdogo wako kwa ajili ya huruma yako hiyo."
Anamshika Mjanja tayari kwa kumchapa kwenye makalio na kumuuliza kwanza,
"Wewe nilikuambiaje kuhusu kuangalia video kwa watu?"
"Nisamehe mamaaa. Nilisahau leo, Juma aliniambia tucheze."
"Wewe kila siku unajidai huelewi eeh. Huko shule utasoma nini kama huelewi kitu?"
Anamchapa na Mjanja kulia kwa kelele kubwa ambazo zinasimamishwa na kukemewa kutoka kwa mamaye akitakwa aache kelele. Baada ya kuridhika na adhabu hiyo, mama Kayumbas anasema
"Na akirudi baba yako nitakusemea. Kama hawezi kuwanunulia tivii ajue namna ya kuwakataza kwenda kukodolea macho za watu."
Baadaye Kayumbas anamueleza mama yake kuhusu kuhitajika kwa shilingi mia mbili kila siku kwa ajili ya masomo ya ziada maarufu kama twisheni kwani walimu wamewaambia kuwa darasa la tano mpaka la saba linahitaji twisheni.
"Sawa mana oko nimekusikia, tutakupa hiyo hela."
Anajibu kwa mkato lakini moyoni anaanza kuwaza kama watakuwa na uwezo huo wa kutoa karibu mia nane kila siku kwa ajili ya shule. Hofu inazidi kumuingia kwamba muda utafika hela hiyo itaongezeka kwani Jennifer naye atahitajika hela ya twisheni pindi akifika darasa la tano na pia muda Mjanja atakapoanza chekechea na Majaliwa kuanza la kwanza.
Mawazo hayo yanamuondoa umakini wake kwenye mambo yanayokuwa yakitokea muda huo na kuamua kwenda chumbani kwake kupumzika kwa muda mpaka akili yake itulie. Akili hiyo inatulia baada ya kutumaini kushauriana na mumewe mambo hayo muda ambao mumewe atarudi kutoka kazini siku hiyo.
Mama Kayumbas anasubiri sana siku hiyo hata inatimu saa tano kasorobo ndipo anaposikia hodi mlangoni kwao. Muda huo watoto wote wanakuwa tayari wakikoroma na anapofungua mlango, kabla hata ya salamu kauli yake ya kwanza inakuwa,
"Mbona umechelewa hivi baba Kayu, imekuwaje huko?"
"Ka...ka..kazi leo iii...ilikuwa ngumu mmma Ka. Tuu..tulikamatwa na...na...na trafiki mmm..mara mbili kwa hiiiyo ii..iii...ikabidi tu...tu...tuongeze ruti ku...ku...kufidia."
"Pole mume wangu, maisha tu hayo. Afu mwanao Kayumbas anahitaji mia mbili ya twisheni kila siku."
"Sasa mm..mmke wangu iii...i..ina ma..ma..maana hilo na...lo uu..uu..unahitaji kuniambia mmimi? Uuu..uuu..we si uuu..mpe tu? Eee? Mm..mi naacha chote nii..nii..patacho mbona?."
"Siyo hivyo baba Kayu, nilikuwa nakuambia tu mume wangu ili ukae ukijua hivyo."
"Sawa, tu..tu..tushirikiane kuu..kuu..hakikisha watoto wetu wa...wa..wana..wana..pata elimu nzuri. Mmm..mmi sijui ni..ni..nitajisss..sikiaje kuu..kuupandisha wa..watoto wa watu kwee..nye gari yangu saa nyiii...ngine bu..bu..bure kabisa ili..ili..ili wakasome haa..ha..halafu waa..wa..wanangu wenyewe sss...siyo wanafunzi."
"Watoto wetu watasoma tu mume wangu, acha sisi tufanye tuwezalo na Iruwa ataweka mkono wake."
Baba Kayumbas anamtazama machoni mama Kayumbas baada ya kusema kauli hiyo na mama Kayumbas anapoona akiangaliwa hivyo, anatabasamu kidogo huku akimpiga kidogo begani baba Kayumbas na kumuambia,
"Na wewee! Haya Mungu ataweka mkono wake."
"Amina." Baba Kayumbas anajibu kwa sauti na kwa haraka.
"Hivi, baba Kayu kwa nini siku hizi hutaki kabisa kunisikia nikiongea maneno ya Kichaga?"
"Uuuu..uunawafanya wa..waa.watoto nnnao waanze ku..ku..kusema maneno ya Kichaga."
"Kwani kuna ubaya gani baba Kayu?"
"Baba yao si...ssssisiyo mmm..mmchaga."
"Basi wafundishe kikwenu."
"Mmmi ssississi..kijui nnnna haina mmmmaana."
"Mmh ya kushindwa hayo. Tuachane na hayo, swala lingine mume wangu ujue ni nini?"
"Enhee nii...ambie!"
"Hebu jitahidi basi mwezi huu uwanunulie wanao tivii na wao waangalie. Ujue watakuwa watumwa kwa ajili ya kuangalia video kwa watu?"
"Ha..haa..pana mke wangu, ti..tii..tivii siyo mu..mu..mu..himu sss...saaana kwa sasa. Waa..waa..wangapi ha..haawana tivii hadi leo? Aa..aangalau uuu..uu..ungeniambia tuujipange ku..ku..kukutafuta ki..ki..kiwanja chetu tuu..tu..kajenga ki..banda kidogo... Mmmi nadhani.."
"Mume wanguu, au kwa vile wewe hushindi hapa nyumbani ndiyo maana huoni karaha yake? Kila muda Mjanja yupo kwa watu anaangalia mapicha, kama mzazi napenda kumuona mwanangu akifurahi kukaa hapa nyumbani siyo kila dakika huyo, churupu kwa watu."
"Bado mmmdogo huyo mmmke wangu, aa..aaa...atakuja kuacha sss..siiku moja. Mmm..mbona wee..weenzake hawa..hawaafanyi hivyo?"
"Siyo kwamba hawapendi, inawauma kukaa hivyo lakini ndiyo wafanyaje na mimi nimewakataza? Tuwanunulie tivii bwana mbona hazina hata bei sana? Kama kuhama tutahama nazo tu."
"Sssaawa mm..mke wangu, ng'..ngoja nianze ku..kuuu..weka hiyo hela basi.”

[Endelea kufuatilia simulizi hili litokanalo na matukio ya kweli...]

1 comment:

  • Hadithi na Simulizi